Arusha
Home » » POLISI ARUSHA YATOA ONYO

POLISI ARUSHA YATOA ONYO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 



Na Rashid Nchimbi wa Jeshi la Polisi Arusha

Jeshi la Polisi mkoani hapa lipo kwenye mkakati wa kuwachukulia hatua viongozi wote wanaoishi au kufanyia kazi katika maeneo ambayo yatabainika wananchi wa maeneo yao wanalima bhangi bila wao kuwachukulia hatua zozote au kutoa taarifa kwa vyombo husika.

Hayo yameelezwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha Naibu kamishna (DCP) Charles Mkumbo alipokuwa anaongea na waandishi wa habari ofisini kwake baada ya operesheni iliyofanyika katikati ya wiki iliyopita katika kijiji cha Kismiri Juu, kata ya Uwiro tarafa ya King’ori wilayani Arumeru,

“Mara kadhaa tunapofanya operesheni hizo wananchi wa eneo hilo huwa wanakimbia na kuacha nyumba zao huku viongozi wao kutoonekana kabisa au kutoa taarifa zozote juu ya uhalifu huo, sasa tutawachukulia hatua kwani wao ni sehemu ya uwajibikaji katika kuzuia vitendo vya uhalifu”. Alisema Kamanda Mkumbo.

Katika operesheni hiyo, jeshi la Polisi lilifanikiwa kupata jumla ya magunia 22 ya bhangi yaliyokuwa yamehifadhiwa katika nyumba za wakazi hao na kwenye makorongo yanayozunguka kijiji hicho pamoja na kilogramu 80 za mbegu za mmea huo ambazo zote ziliharibiwa kwa kuchomwa moto.

Kamanda Mkumbo aliendelea kueleza kwamba, katika operesheni hiyo pia walifanikiwa kumkamata mtuhumiwa mmoja aitwaye Raphael Laizer (33) mkazi wa Kismiri Juu akiwa na magunia matatu ya bhangi huku taratibu za kumfikisha mahakamani zikiwa zinaendelea.

Kamanda Mkumbo aliongeza kwa  kusema kwamba, imekuwa vigumu kuwakamata watuhumiwa kutokana  na  jiografia ya eneo hilo ambapo kila kunapokuwa na operesheni askari wanapokwenda,  wananchi hao wanawaona kirahisi au kusikia miungurumo ya gari na kisha hukimbilia milimani na kuwaacha wazee na watoto.

“Japokuwa operesheni hizo ambazo tunazifanya mara kwa mara zimekuwa za mafanikio lakini changamoto zilizopo ni pamoja na miundo mbinu ya eneo hilo si rafiki kwa magari hasa uwepo wa milima mirefu na ubovu wa barabara”. Alifafanua Kamanda Mkumbo.

Operesheni hiyo iliyofanyika kuanzia saa 12:00 asubuhi mpaka saa 7:30 mchana ilijumuisha askari wa vikosi na vitengo mbalimbali huku ikisimamiwa na Mkuu wa Operesheni mkoani hapa Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) James Manyama.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa