




Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Wakili Julius Mtatiro, ni miongoni mwa wahitimu waliotunukiwa shahada za uzamili katika mahafali yaliyofanyika Ijumaa, Februari 6, 2026, katika Chuo Kikuu cha Uhasibu Arusha (IAA), yaliyofanyika Ngurdoto jijini Arusha.
Katika mahafali hayo, Mtatiro ametunukiwa Shahada ya Uzamili ya Masomo ya Amani na Usalama (Master of Arts in Peace and Security Studies) na kuchaguliwa kuwa msemaji mkuu wa wahitimu wote, ambapo alitoa hotuba kwa niaba yao.
Amesisitiza umuhimu wa vijana kuendelea kujifunza na kujiongezea maarifa kulingana na nafasi na ndoto zao, akieleza kuwa elimu hiyo inapaswa kuendana na mahitaji ya ujuzi, ushindani wa kimataifa pamoja na vipaumbele vya kimkakati vya maendeleo ya Tanzania ya sasa.
Mbali na shahada hiyo mpya ya uzamili, Mtatiro pia anamiliki Stashahada ya Uzamili ya Sheria kwa Vitendo (Postgraduate Diploma in Legal Practice) pamoja na shahada nyingine tatu za uzamili ambazo ni: Uzamili wa Usimamizi wa Umma Uzamili wa Sera za Umma na Uzamili wa Mawasiliano ya Umma.
Aidha, ana shahada mbili za kwanza ambazo ni:vShahada ya Sanaa katika Elimu na Shahada ya Sheria (LL.B).
Akiwa mwanafunzi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Mtatiro anakumbukwa kwa mchango wake katika harakati za wanafunzi zilizoleta mabadiliko katika usimamizi wa sera za elimu ya juu, hususan eneo la mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu.
Katika kipindi hicho, aliwahi kushika nyadhifa mbalimbali za uongozi wa wanafunzi zikiwemo: Waziri wa Mikopo – DARUSO. Waziri Mkuu – DARUSO na Katibu Mkuu – TAHLISO.
Mtatiro pia aliwahi kuwa kiongozi mwandamizi wa Chama cha Wananchi (CUF) kati ya mwaka 2009 na 2017, akihudumu katika nafasi mbalimbali zikiwemo: Mkurugenzi wa Haki za Binadamu na Sheria. Naibu Katibu Mkuu – CUF Tanzania Bara na Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi wa Taifa.
Vilevile, aliwahi kuwa Mjumbe wa Bunge la Katiba kwa kuteuliwa na Rais wa Awamu ya Nne, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete.
Kwa upande wa utumishi wa umma, Mtatiro aliteuliwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Tunduru mwaka 2019, nafasi aliyohudumu hadi mwaka 2024. Kuanzia mwaka 2024 hadi sasa anahudumu kama Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga.
Mbali na majukumu ya kiutawala, Mtatiro anatambulika pia kama mwalimu, wakili, na mchambuzi wa sera za umma mwenye uzoefu mpana katika masuala ya utawala na maendeleo.
Na Pamela Mollel,Arusha
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. CPA Amos Gabriel Makalla, amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeendelea kuimarisha huduma za afya kwa kusogeza huduma za kibingwa za magonjwa ya moyo karibu na wananchi.
Anasema uanzishwaji wa Kituo cha Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) katika Hospitali ya Arusha Lutheran Centre (Seliani) utawanufaisha wananchi wa Arusha na mikoa ya jirani, pamoja na watalii na wageni watakaoshiriki michuano ya AFCON 2027.
Mhe Makalla anayasema hayo wakati wa ziara yake ya kukagua zoezi la utoaji wa vipimo na matibabu ya magonjwa ya moyo bure, ambapo jumla ya wananchi takribani 1,200 wamenufaika na huduma hizo, huku Serikali ikiahidi kuwawezesha wananchi wasiokuwa na uwezo wanaohitaji rufaa ili wapate matibabu zaidi katika Taasisi ya Moyo ya JKCI jijini Dar es Salaam.
Aidha, amewahamasisha wananchi kujiunga na Bima ya Afya kwa Wote ili kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora za afya kwa wakati.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Kisenge, amesema katika Kanda ya Kaskazini, magonjwa ya moyo na magonjwa yasiyoambukiza yameendelea kuonekana kwa kasi, ambapo kupitia programu ya upimaji wa afya, zaidi ya wananchi 3,000 wamejitokeza kupima afya zao.
Anasema kuwa kati yao, asilimia 9 walibainika kuwa na matatizo ya moyo, huku asilimia 29 wakigundulika kuwa na shinikizo la damu, ugonjwa uliokuwa unaongoza zaidi kwa wananchi wenye umri kati ya miaka 45 hadi 80
Dkt. Kisenge ameongeza kuwa sababu kuu zinazosababisha ongezeko la magonjwa hayo ni kutofanya mazoezi ya mwili, unene uliopitiliza, unywaji wa pombe kupita kiasi, uvutaji wa sigara, pamoja na kutokuzingatia lishe bora, akiwahimiza wananchi kubadili mtindo wa maisha na kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara ili kuepuka madhara makubwa ya kiafya.
Na Mwandishi Wetu, Arusha.
Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imeonyesha dhamira ya dhati Kufanya kazi bega kwa bega na wadau wa maendeleo kuhakikisha uboreshaji wa mfumo wa usimamizi wa mafunzo endelevu wa walimu kazini yaani MEWAKA unaboreshwa na kukamilika kwa wakati na kwa ufanisi ili kuwezesha mahitaji ya walimu wa Sekondari.
Akizungumza wakati wa kuhitimisha warsha iliyofanyika kwa muda ya siku mbili ya tarehe 28 na 29 Agosti 2025, ya mapitio ya mfumo wa MEWAKA ulioboreshwa Mratibu wa Mradi kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Bi. Lina Rujweka, alitoa shukrani kwa juhudi na muda uliowekezwa na wadau wote, ikitambua mchango wao muhimu unaotarajiwa kuleta mafanikio makubwa katika utekelezaji wa mradi huu hasa UNESCO na Jamhuri ya Korea kupitia mradi wa ‘’KFIT III wa Transforming Education through ICT in Africa’’ kwa kuendelea kutoa msaada wa kifedha.
Shirika la UNESCO Dar es Salaam, kwa kushirikiana na Taasisi ya Elimu Tanzania (TET), inaendelea na juhudi za uboreshaji mfumo wa MEWAKA ili kuzingatia mahitaji ya walimu wa shule za sekondari.
Ushirikiano huu ulitokana na tathmini ya mahitaji iliyoonyesha kuwa mfumo wa sasa ulikuwa umeundwa mahsusi kwa ajili ya kuwa jukwaa la mafunzo ya maendeleo ya kitaaluma kwa walimu wa shule za msingi.
Hivyo, wadau walikutanishwa ili kupitia toleo la awali la mfumo wa MEWAKA kwa lengo la kuhakikisha umuhimu, ubora, na uendelevu wa muda mrefu wa jukwaa hilo.
Wadau hao walikuwa kutoka wizara ya elimu, sayansi na Teknolojia , Ofisi ya Rais – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Taasisi ya Elimu Tanzania, Tume ya Kitaifa ya UNESCO na baadhi ya walimu wa shule za sekondari.
Katika hotuba yake ya ufunguzi, mwakilishi kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Ally Mape alisema majukwaa ya kidijitali ni nyenzo yenye nguvu ya maendeleo ya kitaaluma, yanayochangia kwa kiasi kikubwa kuwawezesha walimu kupata ujuzi na kujiamini ili kufanikisha kazi zao katika Dunia ya sasa.
Kwa upande wake mkuu wa Sekta ya Elimu kutoka Ofisi ya UNESCO Dar es Salaam, Dkt. Faith Shayo, ameeleza kuwa lengo kuu ni kupanua upatikanaji wa mafunzo endelevu ya kitaaluma kupitia majukwaa ya kidijitali, hivyo itasaidia kuboresha matokeo ya ufundishaji na ujifunzaji kote nchini.
Hata hivyo Dkt. Shayo aliwahimiza wadau kutoa maoni na mitazamo yao kusaidia kuhakikisha toleo la mwisho la mfumo huu sio tu kuwa la kisasa bali pia rahisi kutumia na lenye matokeo chanya.
Mpango huu unalingana na juhudi za Serikali za kuunganisha TEHAMA katika elimu, kama inavyoonekana katika sera na mikakati muhimu ya kitaifa ikiwemo Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 toleo la 2023, Mkakati wa Kitaifa wa Elimu ya Kidijitali 2025 – 2030, Dira ya Maendeleo ya 2050, Mitaala ya Elimu ya Msingi na ya Ualimu, pamoja na mipango ya kimataifa kama vile Malengo ya Maendeleo Endelevu hasa lengo namba nne.