Arusha
Home » » TANZANITE YAVUSHWA KENYA BILA KODI

TANZANITE YAVUSHWA KENYA BILA KODI

na David Frank, Namanga
SERIKALI inapoteza mamilioni ya shilingi kutokana na shehena ya zaidi ya tani mbili za madini ya Tanzanite yanayochimbwa Mirerani, wilayani Simanjiro, Manyara, kutoroshwa kupitia mpaka wa Namanga kwenda nchini Kenya kila mwaka bila kulipiwa kodi.

Hayo yalibainishwa jana na kamishna msaidizi wa madini kanda ya kaskazini, Benjamin Mchwampaka, akisema hali hiyo imetokana na Kenya kuendelea kutumia sheria za zamani za madini ambapo wafanyabiashara hawalazimiki kulipa kodi au mrahaba kwa mauzo ya nje ya madini au vito vya thamani.

Mchwampaka alisema kuwa baada ya serikali kubaini kuwepo kwa utoroshaji huo, ilichukua hatua madhubutu ambapo walikutana na maofisa wa madini wa serikali ya Kenya na kuafikiana katika mambo mbalimbali ikiwemo suala la ulipaji kodi na njia za kudhibiti uingiaji holela wa madini nchini humo.

“Tulikuwa na kikao na wenzetu akiwemo kamishna wa madini wa Kenya na kimsingi alikiri kuwa nchi yake husafirisha nje madini ya Tanzanite yenye uzito wa wastani wa tani mbili kila mwaka na katika kipindi cha 2012 madini yapatayo tani 2.15 yalipitia Nairobi kwenda nje ya nchi,” alisema.

Inadaiwa kuwa wafanyabiashara wengi wa Tanzania hupendelea kusafirisha Tanzanite kupitia Kenya kwa sababu huwa hawalazimiki kulipa kodi, tofauti na ikiwa wangeamua kuyauza madini hayo adimu kutokea nchini hapa.

Thamani ya Tanzanite katika soko la ulimwengu hususan Marekani ni mara-kumi zaidi ya ile ya almasi na madini haya ya bluu hupatikana eneo la Mererani pekee lakini hadi sasa ni nchi ya India katika mji wa Jaipuri ndiyo inadaiwa kufaidika na madini hayo ambayo katika miaka ya nyuma yalihusishwa na mtandao wa kigaidi wa Osama Bin Laden.

Akizungumza kuhusu sheria za umiliki na usafirishaji wa madini Tanzania kwa maafisa wa polisi, forodha, uhamiaji na usalama katika mji mdogo wa Namanga, Mchwampaka aliongeza kuwa kwa kipindi cha mwaka jana Kenya ilijipatia wastani wa sh milioni 73 ambazo ni sawa na sh bilioni 1.5 za Kitanzania katika kusafirisha na kuuza Tanzanite nje.

Tanzania hutoza kati ya dola za Kimarekani 200 na 2000 zikiwa ni kodi za kusafirisha madini nje na kodi hizi hutofautiana kati ya wazawa, wageni na watalii pamoja na aina au idadi ya madini husika.

Mkuu wa wilaya ya Longido, James Ole Milia, akifungua mkutano huo aliwataka watendaji wote walioshiriki semina hiyo kutekeleza majukumu yao kwa weledi ili kulinda rasilimali za nchi zisitoroshwe kwenda nje kiholela na hivyo kuikosesha mapato serikali.


SOURCE TANZANIA DAIMA

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa