Arusha
Home » » Majaliwa asisitiza utunzaji rasilimali

Majaliwa asisitiza utunzaji rasilimali

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akipokea vitabu kutoka kwa Rais wa Bermuda Emmissions Control Limited, Donal Smith katika mkutano wa Africa World Heritage alioufungua kwenye Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) jijini Arusha jana. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).
WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amewataka wataalamu wa mambo ya malikale na uhifadhi wa urithi asilia, watafute mbinu zitakazoimarisha utunzaji wa rasilimali hizo bila kuathiri mifumo ya uchumi ya nchi zinazoendelea.
Alitoa mwito huo jana wakati akifungua Mkutano wa Kimataifa wa siku nne unaojadili Uhifadhi wa Urithi wa Dunia wa Afrika kama nyenzo ya kuleta maendeleo endelevu ulioanza jana kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Arusha (AICC) jijini Arusha.
Waziri Mkuu alisema kuna baadhi ya nchi ambazo ni masikini, lakini zimebarikiwa kuwa na rasilimali kama madini na gesi asilia, lakini kwa sababu rasilimali hizo ziko karibu sana na vivutio vya urithi asilia wa dunia, watu wa nchi hizo wanazuiwa kuchuma rasilimali zao ili wasiharibu vivutio hivyo.
“Tunatambua umuhimu wa kutunza rasilimali na vivutio vya urithi asilia. Hivi ni kwa nini zisitafutwe teknolojia zinazofaa ambazo zitaruhusu uvunaji wa gesi asilia na madini bila kuathiri uhifadhi wa vivutio vya urithi asilia wa dunia (world heritage sites)?” Alihoji Waziri Mkuu.
“Serikali za nchi za Kiafrika zinahitaji suluhisho kama hili wakati zikiendelea kutafuta njia sahihi za kuwianisha uhifadhi wa vivutio vya urithi wa dunia na changamoto ya kuondoa umasikini miongoni mwa wananchi wake,” alisema.
“Sisi viongozi ambao wengi wetu ni wanasiasa, hatukatai ushauri wa wataalamu lakini tunawasihi baadhi yenu ambao mnashiriki mkutano huu muhimu, mtafute njia mbadala za kufumbua tatizo hili badala ya kuendelea kutegemea njia za kizamani za kukabiliana na changamoto kama hizi ili sote tuweze kunufaika na rasilimali zilizopo ikiwa ni pamoja na kutunza vivutio vya urithi asilia wa dunia,” aliongeza.
Chanzo Gezeti La Habari Leo

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa