Arusha
Home » » ARUSHA YAZIDI KUDHIBITI MADAWA YA KULEVYA

ARUSHA YAZIDI KUDHIBITI MADAWA YA KULEVYA

 
Na Rashid Nchimbi wa Jeshi la Polisi Arusha
Jeshi la Polisi Mkoani hapa limeendelea kupambana na wahalifu wa madawa ya kulevya ambapo juzi limefanikiwa kukamata magunia 20 ya madawa hayo aina ya bangi.
Akizungumzia tukio hilo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Liberatus Sabas alisema kwamba, madawa hayo yalikamatwa tarehe 23.07.2014 muda wa saa 2:30 usiku wilayani Longido katika kijiji kiitwacho Olteres.
Kamanda Sabas alisema kwamba, mafanikio hayo yalipatikana baada ya Jeshi hilo kupata taarifa toka kwa raia wema zikieleza kwamba kuna watu wanayasafirisha kwa kutumia wanyama aina ya Punda.
Mara baada ya taarifa hiyo ndipo askari wa Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na askari wa kampuni ya Jumuiya ya Jamii inayojishughulisha na Ulinzi wa wanyamapori na mazingira kambi ya Enduimet walianza kuwafuatilia kuanzia saa 8:00 Mchana na kufanikiwa kuona nyayo za punda pamoja na binadamu ambazo zilikuwa zinaonyesha zimetokea Oldonyasambu kuelekea Namanga.
Kamanda Sabas aliongeza kwa kusema kwamba uchunguzi wa Jeshi la Polisi ulibaini kwamba magunia hayo yanayokadiriwa kuwa na kilogramu 80 kila mojawapo yalikuwa yanapelekwa nchi jirani ya Kenya yalipatikana baada ya msako uliofanywa na askari hao kwa takriba saa 4 na dakika 30 ambapo yalikuwa yametelekezwa kijijini hapo huku wahusika wakitoweka kusikojulikana.
Hata hivyo Jeshi hilo Mkoani hapa linaendelea na upelelezi juu ya tukio hilo ikiwa ni pamoja na kuwasaka watuhumiwa wa tukio hilo huku doria ikiendelea ili kuweza kudhibiti wahalifu wote wanaodhubutu kupita njia za panya baada ya kuona wanabanwa katika barabara kuu.
Jeshi la Polisi mkoani hapa linaendelea kutoa shukrani kwa wananchi wanaotoa taarifa za mara kwa mara juu ya uhalifu na wahalifu na kuomba waendelee kujitokeza ili taarifa hizo zifanyiwe kazi na hatimaye kufanikisha kupunguza uhalifu wa maeneo mbalimbali ya Mkoa huu.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa