Home » » BARAZA LA MADIWANI ARUSHA LAWAVAA WAALIMU WAKUU

BARAZA LA MADIWANI ARUSHA LAWAVAA WAALIMU WAKUU

BARAZA la Madiwani la Halmashauri ya Jiji la Arusha jana lilikuja juu na kutaka kauli kutolewa juu ya ni hatua gani zichukuliwe kuhusu walimu wakuu wa shule za msingi na sekondari wanaowachangisha wazazi fedha kabla ya mtoto kuanza darasa la kwanza na wanaojiunga kidato cha kwanza.
Diwani wa TLP, Michael Kivuyo ndiye aliyeanzisha mjadala huo kwa kutoa hoja binafsi iliyoungwa mkono na karibu madiwani wote na kusema kuwa watoto wanarudishwa shule iwapo hawatakuwa wametoa kiasi cha fedha kinachopangwa na Mwalimu Mkuu.
Kivuyo alisema mbali ya hilo hata mtoto aliyefanikiwa kufaulu na kuingia Kidato cha Kwanza naye ana michango yake na iwapo michango hiyo haitatolewa na wazazi, watoto hawaruhusiwi kuanza shule ya msingi na kidato cha kwanza.
Alisema na kuwaeleza Madiwani kuwa; “watoto wanarudishwa shule na walimu wakuu kwa kushindwa kulipa michango hiyo ambayo sijui fedha zake zinafanya nini na zinaingia katika fungu lipi kwani Serikali ilishapiga marufuku suala la michango holela isiyokuwa ya kisheria.”
Diwani huyo alisema kuwa Baraza la Madiwani limekuwa likiagiza kila mara katika vikao vyake juu ya walimu wakuu kuacha mara moja kuchangisha wazazi michango hiyo lakini walimu hao wakuu wamekuwa wajeuri na wakaidi kwa kushindwa kutekeleza amri na maagizo ya Baraza tangu mwaka juzi na aliliomba Baraza kutoa kauli juu ya hilo ili iwe mwisho kwa walimu kuchangisha.
‘’Walimu wakuu wamekuwa miungu mtu kwani wanachangisha fedha bila ya utaratibu na wanawarudisha watoto majumbani ambao wanashindwa kutoa michango hiyo hivyo naomba Baraza kutoa kauli juu ya walimu wakuu,’’ alisema.
Naye Diwani wa Sekei kupitia Chadema, Crispin Tarimo yeye alioneshwa kusikitishwa na hali hiyo na kusema kuwa wananchi wameshoshwa na michango hiyo isiyokuwa na utaratibu na kuwataka madiwani kuiunga hoja hiyo na kutolea maamuzi mazito juu ya walimu wakuu wenye tabia ya kukaidi amri ya Baraza na Serikali Kuu.
Tarimo aliendelea kusema Serikali Kuu iliagiza kuwa hakuna mtoto atakayerudishwa shule kwa kukosa michango na Baraza la Jiji la Arusha katika vikao vyake liliagiza hivyo hivyo lakini agizo hilo limeshindwa kutekelezwa na walimu wakuu wa shule za msingi na sekondari za Jiji la Arusha.
Diwani wa Lemara CCM, Karimu Mushi alizungumza kwa masikitiko makubwa na kusema kuwa wazazi na wananchi wanabebeshwa mzigo mkubwa ambao hauko kisheria hivyo aliomba Baraza kuangalia hilo kwa faida ya baadaye.
Diwani wa Terrat CCM , Julius ole Sekayani yeye aliwaunga mkono madiwani wote walitoa hoja na kuchangia na kumtaka Mstahiki Meya wa Jiji la Arusha, Gaudence Lyimo na Baraza kuthubutu kuchukua hatua juu ya ukaidi wa walimu wakuu hao.
Akizungumzia kauli za madiwani hao, Meya Lyimo alimtaka Mwenyekiti wa Kamati ya Elimu, Afya na Uchumi kuchukua hoja hizo na kuzifanyia kazi na kutoa taarifa katika kikao kijacho cha Baraza uamuzi ambao baadhi ya madiwani walionekana kuupinga. Meya Lyimo alisema; “
Hata mimi suala hili la walimu wakuu kukaidi linanisikitisha na hapa nataka kujiridhisha zaidi, naomba niipe kazi kamati hiyo ifanye kazi na kutoa mapendekezo katika kikao kijacho.”
Chanzo;Habari Leo

0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa