Arusha
Home » » Kituo cha tiba za asili kutoka Austria chaja

Kituo cha tiba za asili kutoka Austria chaja



MKURUGENZI wa Kampuni ya  Afrika Amini Alama iliyopo katika Hifadhi ya Momela jijini Arusha, Dk. Christine Wallner,   amesema kuwa wana mpango wa kuanzisha kituo cha tiba ya asili, ikiwa ni mbinu mpya za matibabu ya asili  kutoka nchini Austria, ambayo itawasaidia wagonjwa wengi wakiwamo wa ukimwi.
Kituo hicho maalumu kwa tiba ya asili kinatarajiwa kuwasaidia wana jamii ya Wamasai na Wameru wanaoishi katika vijiji vya Ngabobo na Ngarenanyuki, Mkoa wa Arusha  na mikoa mingine na hata nchi jirani.
Tayari taratibu za kuanzisha kituo hicho zimeshaanza, ikiwamo kupeleka maombi katika Wizara ya Afya na kupata eneo ambalo litatumika kujenga kituo hicho pamoja na wataalamu waliobobea katika fani hiyo.
Dk. Christina akizungumza na waandishi wa habari, alisema kuwa kituo hicho kitasaidia wagonjwa wa mifupa, uti wa mgongo na kuwasaidia wagonjwa wa ukimwi kuimarika kiafya.
“Tunahitaji kufanya kazi pamoja na serikali kwani imekuwa ikiridhia jitihada tunazozifanya hata tulipoanza na ujenzi wa zahanati  ya kijiji ambayo ina chumba kidogo cha upasuaji, wodi na leba, ambapo tayari imeanza kutumika,” alisema Dk. Christine.
Mbali na hayo, mkurugenzi huyo ameweza kujenga Shule ya Masai Vision Primary School, Afrika Amini Sports Academy, kituo cha afya, Afrika Amini Training Center na kuanzisha kikundi cha Umoja wa Kina Mama Wazalishaji (Women Group).
Kwa upande wake, Dk. Christine alisema kuwa miradi ya maendeleo ya jamii iliyoanzishwa imewasaidia watoto 550 kusoma bure na kupata udhamini wa mahitaji yao muhimu kama chakula, malazi na vifaa vya shule na bado wanaendelea kuangalia namna ya kuisaidia jamii inayowazunguka na vijiji vya jirani.

chanzo;tanzania daima



0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa