Arusha
Home » » WAKILI MWALE ASOMEWA MASHITAKA 42 TENA

WAKILI MWALE ASOMEWA MASHITAKA 42 TENA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Imeandikwa na John Mhala, Arusha
WAKILI maarufu jijini Arusha, Mediam Mwale na wenzake watatu jana walisomewa mashitaka 42 kwa mara ya nne katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Arusha.
Mwale anayemiliki Kampuni ya Uwakili ya JJ Mwale Advocates na wenzake watatu, awali walisomewa mashitaka mapya 44 ya utakatishaji fedha haramu, kula njama na kughushi baadhi ya nyaraka na kujipatia kiasi cha cha dola za Marekani milioni 18 sawa na zaidi ya Sh bilioni 40. Lakini jana walisomewa mashitaka 42 mbele ya Hakimu Mkazi, Nestory Baro baada ya kesi hiyo kuondolewa Mahakama Kuu juzi na washitakiwa kukamatwa tena.
Mbali ya Mwale, wengine walioshitakiwa ni Meneja wa Benki ya CRDB tawi la Mapato jijini Arusha, Boniface Thomas, mfanyabiashara wa jijini Nairobi, Kenya, DonBosco Gichana “Bob James Onderi” na Elias Ndejembi. Akiwasomea mashitaka kwa nyakati tofauti, Mwendesha Mashitaka wa Serikali, Shedrack Kimani na Oswald Tibabyakyoma, walidai kuwa kwa nyakati tofauti kati ya mwaka 2010 na 2011 washitakiwa hao walitenda makosa hayo na kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu.
Hata hivyo, Mwale na wenzake walikana mashitaka hayo na kuiomba mahakama kuieleza Jamhuri kuacha danadana katika kesi hiyo na katika mambo ya kisheria, kwani mahakama za juu zilishaifuta kesi kwa zaidi ya mara tatu, lakini Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) amekuwa akiiondoa na kuirudisha tena kwa makosa yale yale.
“Mheshimiwa hakimu kesi hii imefutwa mara tatu na Mahakama Kuu na jana (juzi) Jaji David Mrango aliungana na DPP kuiondoa kesi hii, lakini alionya kuacha kuirudisha tena kwani watuhumiwa wamekaa rumande kwa zaidi ya miaka sita hivyo watende haki,” alidai Mwale.
Baada ya hali hiyo, Mwendesha Mashitaka wa Serikali, Tibabyakyoma alidai upelelezi wa kesi hiyo umekamilika na aliomba tarehe ya kuanza kusikilizwa. Hakimu Baro alisema kesi hiyo itaanza kusikilizwa kesho na mawakili wa utetezi na wa Serikali walitakiwa kujiandaa kwani kesi hiyo itasikilizwa mwezi mzima. Mwale na wenzake wanatetewa na mawakili Albert Msando, Innocent Mwanga, Julieth Tarimo na Omary Omary na Mawakili wa Serikali mbali ya Tibabyakoma, ni Pius Hilla na Shedrack Kimani.
CHANZO HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa