Arusha
Home » » Huduma za Afya kusogezwa kwa wananchi wa Muriet -Arusha

Huduma za Afya kusogezwa kwa wananchi wa Muriet -Arusha

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Nteghenjwa Hosseah, Arusha


Wakazi zaidi ya 27,000 wa kata ya Murriet iliyopo Jiji la Arusha wataondokana na adha ya kutembea umbali mrefu wa zaidi ya km 15 kusaka huduma ya Afya na kujifungua kwa akina mama baada ya Mkuu wa wilaya ya Arusha, Mhe. Gabriel Daqarro kuzindua ujenzi wa Kituo cha Afya kitakachogharimu zaidi ya shilingi milioni 400 katika kata hiyo.
 Kuanza kwa ujenzi wa Kituo cha Afya kitakachokuwa cha kisasa ni kufuatia malalamiko ya muda mrefu ya wananchi wa eneo hilo kwa Waziri Mkuu, Kassimu Majaliwa alipokuwa katika ziara Mkoani Arusha hususani katika Jiji la Arusha kuwa kata hiyo yenye wakazi hao haina zahanati wala kituo cha afya cha uhakika na kufikia hatua ya akina mama kujifungulia nyumbani au njiani wakati wakienda katika kituo cha Afya za Levolosi kilichopo umbali wa km 15 .
 Kufuatia malalamiko hayo ya akina mama waliokuwa na mabango yenye ujumbe mbalimbali ya kutaka kituo cha afya au zahanati,Waziri Mkuu Majaliwa aliagiza mara moja huduma hiyo kuwafikia wananchi bila ya kuchelewa.
Mhe. Daqarro alisema kuanza kwa ujenzi wa kituo hicho ni kufuatia jitihada za Mkuu wa Mkoa wa Arusha,Mhe. Mrisho Gambo kutoa msaada wa vifaa vya ujenzi kama vile matofali 3, 000, mifuko ya sementi 100 na bati 100 kwa ajili ya ujenzi huo.
 Alisema na kuwataka  Halmashauri ya Jiji kwa kushirikiana na  wananchi wa kata hiyo kufanya kila linalowezekana kuhakikisha Kituo hicho cha Afya hiyo kinakuwa na maabara,  chumba cha Upasuaji pamoja chumba cha wagonjwa wa nje sambamba na vifaa vya kisasa ili wananchi waliokuwa katika kata hiyo kupata huduma na kuondokana na adha ya kusafiri umbali mrefu.
Naye Mkurugunezi wa Jiji Ndg. Athumani Kihamia alisema Rais Dkt. John Magufuli katika kipindi cha kampeni aliahidi kila kata kote nchini kuwa na zahanati au kituo cha afya cha  uhakika kwa ajili ya kusongeza huduma ya afya kwa wananchi hivyo Jiji la Arusha limeanza kutekeleza Ahadi hiyo .
Mganga Mkuu wa Jiji la Arusha Dr. Bakari Salumu alisema kuwa Jiji la Arusha linaupungufu wa vituo vya Afya 9 na zahanati 11 kwani vilivyopo havikithi mahitaji ya wananchi kwa sasa.
Dr. Bakari aliongeza kuwa  kwa sasa Jiji la Arusha lina zahanati 71 na vituo vya afya 16 mahitaji ambayo bado hayakithi matwaka ya wakazi wa Jiji hilo lenye mitaa 154 ambalo linakuwa siku hadi siku.
Alisema Kituo hicho cha Afya kinachojengwa kitakuwa na vifaa vyote muhimu na madaktari wa kutosha kutoa huduma hiyo kwani kata hiyo ndio yenye wakazi wengi kuliko kata yoyote katika Jiji la Arusha.

 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa