Arusha
Home » » Lema akwama tena kupata dhamana

Lema akwama tena kupata dhamana

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Mbunge wa Arusha Mjini, Gobless Lema
KIU ya Mbunge wa Arusha Mjini, Gobless Lema kupata dhamana na kujinasua kwenye mkono wa sheria baada ya kusota mahabusu kwa wiki nne sasa, inazidi kufifia baada ya mawakili upande wa serikali kuwasilisha pingamizi la rufaa ya mbunge huyo kusikilizwa katika Mahakama Kuu Kanda ya Arusha.
Lema alishindwa kuingizwa katika chumba cha Mahakama kwa ajili ya kusikiliza kesi yake, badala yake kwa muda wote tangu saa 2:14 asubuhi hadi saa 6:18 mchana alikuwa mahabusu tu akisubiri kupelekwa mahakamani na ndipo baada ya muda, alipanda basi dogo la Magereza kwenda Mahabusu ya Kisongo ambako amekuwapo kwa zaidi ya siku 26 sasa kutokana na kukwama kisheria kupata dhamana.
Rufaa hiyo imepingwa na mawakili wa Serikali ambao ni Paulo Kadushi na Matereus Marandu wakidai kuwa rufaa iliyokatwa na mawakili wa Lema haijakidhi matakwa ya kisheria kwa sababu mawakili hao walikata rufaa badala ya kuonesha kusudio la kukata rufaa.
Materu alisema wamewasilisha pingamizi zao mbele ya Jaji Fatma Masengi ya kupinga Mahakama Kuu kutosikiliza kesi ya dhamana kwa sababu mawakili wanaomtetea Lema ambao ni Peter Kibatala na Sheck Mfinanga, wamekosea kukata rufaa badala ya kuwasilisha notisi ya kusudio la kukata rufaa ndani ya siku 10 baada ya awali Jaji kutupa ombi la kusikilizwa kwa rufaa hiyo.
“Sisi leo tumeweka pingamizi la kusikilizwa kwa kesi hii sababu hawa wenzetu wamekosea wao badala ya kuwasilisha pingamizi la kukata rufaa wakakimbilia kukata rufaa na sheria haisemi hivyo lazima kwanza uoneshe nia ya kukata rufaa ndipo ukate rufaa,” alieleza Materu.
Hivyo pingamizi la kusudio la kukata rufaa litawasilishwa kwa maandishi kesho Novemba 30, mwaka huu saa 2:00 asubuhi, upande wa serikali utawasilisha kwa maandishi hoja zao na saa sita mchana siku hiyo hiyo, na upande wa mawakili wa Lema utajibu hoja za mawakili hao kwa maandishi na Jaji, Masengi atapitia hoja hizo saa tisa alasiri.
Kisha Jaji Masengi atatoa uamuzi dhidi ya pingamizi hilo Desemba 2, mwaka huu na endapo atakubaliana na upande wa serikali upande wa Lema utakuwa umeshindwa na endapo hoja za Lema zikishinda dhidi ya pingamizi la serikali, kesi ya msingi ya kusikilizwa kwa maombi ya dhamana ya mbunge huyo itasikilizwa na kutolewa uamuzi.
Mawakili wa mbunge huyo wakiongozwa na Kibatala, walisema wao awali walisajili maombi ya rufaa namba 112/113 ya mwaka 2016 Mahakama Kuu Kanda ya Arusha ili kudai haki ya dhamana ya Lema aliyonyimwa kutokana na makosa ya kisheria yaliyofanywa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha.
CHANZO HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa