Arusha
Home » » WATAKIWA KUSAMBAZA MBEGU HARAKA

WATAKIWA KUSAMBAZA MBEGU HARAKA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

WANANCHI wa kijiji cha Naadare, kata ya Kitumbeine, wilayani Longido mkoani Arusha, wametoa rai kwa wasambazaji wa mbegu kwa ajili ya kilimo wazisambaze haraka na kwa wakati ili wawahi kupanda.
Aidha, wametoa rai kwa serikali kuangalia uwezekano wa kujengwa shule karibu na maeneo wanayoishi ili kuepuka wanafunzi kutembea zaidi ya saa nne kwenda kupata elimu na kurudi nyumbani usiku.
Rai hiyo ilitolewa na wananchi hao jana wakati wa mkutano wa hadhara pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo anayetembelea wilaya hiyo na kujua kero mbalimbali zinazowakabili.
Mmoja kati ya wananchi hao, Elihuruma ole Sapuk alisema hivi sasa wananchi wa maeneo hayo wanakosa mbegu kwa wakati na kusababisha kushindwa kupanda kwa wakati na hivyo kuvuna mavuno kidogo.
Mwanafunzi, Elisupak ole Sapuk anayesoma shule ya msingi Lorienito alisema, ili afike shuleni mapema analazimika kutoka nyumbani saa 11:00 alfajiri na kufika shuleni saa 4:00 asubuhi, akiwa amechoka kutokana na kutembea umbali mrefu.
Alisema na akitoa nyumbani alfajiri anakuwa hajala chakula hivyo ni vyema sasa wazazi na walezi kuchangia elimu ili wanafunzi waweze kusoma kwenye maeneo yaliyo karibu na nyumbani kwao.
Mwananchi Elizabeth Senate alisema, wameamua kukusanya nguvu zao kwa ajili ya ujenzi wa madarasa matatu eneo hilo, lakini wameshindwa jinsi ya kupaua na kuweka huduma nyingine muhimu ili kupunguza umbali mrefu watoto wao wanaotumia kutafuta elimu.
Gambo alisema amesikia kero ya elimu kwa watoto hao na kuahidi kutafuta mabati na mahitaji mengine kumaliza kupaua jengo hilo la shule.
Mkuu wa Wilaya ya Longido, Daniel Chongolo alisisitiza Wakala wa Mbegu kusambaza mbegu kwa wakati kwa wananchi hao ili walime na kupata mazao mengi yatakayowasaidia kukabiliana na ukosefu wa chakula. CHANZO:HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa