Arusha
Home » » Viongozi Kurugenzi Saccos watumbuliwa

Viongozi Kurugenzi Saccos watumbuliwa

UONGOZI wa Mkoa wa Arusha umeisimamisha kazi Bodi na Menejimenti ya Chama cha Kuweka na Kukopa (Saccos) ya Kurugenzi Saccos kilicho chini ya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa kwa tuhuma za ufisadi na imeagizwa wahusika kufikishwa mahakamani.
Taarifa ilitolewa jana na Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Richard Kwitega, ilieleza kuwa bodi hiyo na menejimenti yake, imesimamishwa kazi kutokana na tuhuma za ufisadi wa mfuko wa wanachama wa Saccos hiyo wenye thamani ya Sh milioni 600.
Kwitega alisema amemuagiza Kaimu Mrajisi wa Vyama vya Ushirika mkoa wa Arusha, Nerei Kyara, kuchukua hatua za kisheria kwa kuwafikisha mahakamani watuhumiwa wote.
Pia Kwitega ameagiza kuchukuliwa taratibu zinazohusiana na sheria ya vyama vya ushirika, ikiwa ni pamoja na kuitisha mkutano mkuu maalumu wa wanachama wa Saccos hiyo.
Alisema hatua hiyo imechukuliwa baada ya idadi kubwa ya wanachama kulalamika kutokupewa mikopo pia mikopo kutolewa kinyume cha taratibu kwa taasisi binafsi, tofauti na utaratibu wa Saccos unavyoelekeza.
Aliwataja waliosimamishwa kuwa ni Mwenyekiti wa Bodi, Dk Freedom Makiago kutoka Hospitali ya Mkoa ya Mount Meru na wakurugenzi wa bodi hiyo, Meneja wa Saccos hiyo, Christine Sumaye na Menejimenti.
Katibu tawala huyo alitoa muda wa siku 10 kwa Mrajisi wa Vyama vya Ushirika mkoa wa Arusha, kuanzia juzi kuchukua hatua kumaliza mgogoro huo.
Alisema Kurugenzi Saccos inadaiwa mamilioni ya fedha kutoka kwa taasisi za fedha, kama vile benki ya CRDB na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF).
Hivi karibuni wanachama wa Kurugenzi Saccos kwenye mkutano mkuu maalumu uliofanyika mwezi uliopita, walimuomba Katibu Tawala wa Mkoa kusitisha makato ya mishahara yao kulipia mikopo kwenye chama hicho kwa kuwa hawakuelewa hatima ya fedha zao.
Wanachama hao wakiwemo wastaafu wa Hospitali ya Mount Meru, walisema kwa kipindi kirefu Bodi ya Mikopo ya Saccos hiyo, imeshindwa kuwakopesha kwa kukiuka taratibu za taasisi za fedha.
HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa