Arusha
Home » » Wafugaji wanaoishi ndani ya hifadhi ya Ngorogoro kutoondolewa

Wafugaji wanaoishi ndani ya hifadhi ya Ngorogoro kutoondolewa

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

MKUU wa Mkoa wa Arusha, Felix Ntibenda amesema kuwa serikali haina mpango wa kuwaondoa wafugaji wa jamii ya kimasai wanaoishi ndani ya Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro.
Aidha amesema serikali itahakikisha inawalinda na kuwapatia kila kinachostahili kama wananchi wengine, ikiwemo chakula cha msaada.
Ntibenda alisema hayo katika kijiji cha Inokanoka kilichopo wilayani Ngorongoro na kusema kuwa propaganda zinazoenezwa kuwa serikali inataka kuwatimua hazina ukweli wowote.
“Nimesema serikali haina mpango wa kuwahamisha wananchi wanaoishi ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro kwa kuwa wana haki ya kuishi kwenye eneo hilo,’’ alisema na kuongeza: “Kutokana na hali hiyo, nimeagiza tani 1,000 za mahindi ziletwe hapa ili kupunguza uhaba wa chakula unaowakabili.’’
Alisema uvumi unaoenezwa na watu wasioitakia mema nchi unapaswa kupuuzwa, kwani serikali ya Rais John Magufuli inapenda wananchi wake na haiwezi kamwe kuwaondoa katika eneo hilo.
Mkuu wa wilaya ya Ngorongoro, Hashim Mgandila alisema kumekuwa na kauli zinazotolewa na baadhi ya watu wenye lengo la kugombanisha wananchi na serikali yao juu ya eneo hilo.
Mgandila alisema kwa kauli iliyotolewa na Mkuu wa Mkoa juu ya kuendelea kukaa ndani ya hifadhi kwa wafugaji wa jamii ya kimasai itasaidia kwa kiasi kikubwa wakazi hao sasa kufanya maendeleo badala ya kukaa kwa wasiwasi kama watakuwepo ama la.
Akizungumzia upungufu wa chakula, Kaimu Mkuu wa kitengo cha maendeleo ya jamii wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro, Kuya Sayaleki alisema mamlaka imeshaagiza tani 12,000 za mahindi kukabiliana na upungufu wa chakula kwa wakazi wa ndani ya hifadhi hiyo.
Sayaleki alisema kamwe Mamlaka ya Hifadhi haiwezi kuona wananchi waliopo ndani ya hifadhi hiyo wakikabiliwa na njaa wakati wana uwezo wa kutatua tatizo hilo.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa