Mkufunzi
ambaye pia ni mtaalamu mshauri wa Unesco, katika masuala ya utalii
endelevu, James Banks akiendesha mafunzo kwenye warsha ya siku nne ya
kutengeneza mkakati wa utalii endelevu hifadhi ya Ngorongoro
iliyomalizika mwishoni mwa wiki mji mdogo wa Karatu, mkoani Arusha na
kuandaliwa na Shirika la UNESCO kwa kushirikiana na Ngorongoro
Conservation Area Authority (NCAA). Pichani chini kulia ni Mmoja wa
wakufunzi wa warsha hiyo, Tamim Amijee.(Picha zote na Zainul Mzige wa modewjiblog)
Na modewjiblog, Karatu
SHIRIKA
la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO)
likishirikiana na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) wameandaa
kongamano la siku nne lililofanyika mjini hapa kuangalia mkakati mpya wa
kuendeleza utalii kama kitovu cha mapato katika hifadhi ya Ngorongoro.
Kongamano
hilo ni moja ya makongamano kadhaa ambayo yameandaliwa kwa pamoja kwa
lengo la kutoa mwelekeo mpya katika hifadhi hiyo ambayo binadamu na
wanyama huishi pamoja.
Akizungumza
na mtandao huu Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la elimu
sayansi na utamaduni (UNESCO), Zulmira Rodrigues, alisema kwamba
kongamano hilo limeandaliwa kwa lengo la kujenga uwezo kwa wadau
mbalimbali wa sekta ya utalii kutambua haja ya utalii endelevu ambao pia
utazingatia maslahi ya wananchi wanaoishi katika eneo hilo.
Alisema
wakati NCAA inaangalia upya mkakati wake wa maendeleo katika hifadhi
hiyo ambayo pia ni urithi wa dunia, UNESCO kama washirika wa karibu
wamekubaliana kuendesha kongamano ambapo wadau wote kuanzia wananchi
wanaoishi katika hifadhi hiyo na waendesha utalii zikiwemo hoteli na
watawala kuangalia namna bora ya kuendesha hifadhi na kuneemesha
wananchi.
Zulmira
alisema kwamba hifadhi hiyo inaingiza fedha nyingi ambazo zingeweza pia
kuwafikia wananchi moja kwa moja kwa kuanzisha mikakati ambayo
inahusisha wananchi wenyewe na wadua mbalimbali wa sekta hiyo.
Alisema
kwamba idadi ya watalii wanaoingia hapo wanaingiza fedha nyingi
serikali kuu lakini kiasi hicho hakionekani wazi wazi kwa wananchi na
hivyo ipo haja ya kuangalia mwelekeo mpya ambao utaendelea kuhifadhi
urithi huo huku wananchi wake wakifaidika na uwapo wa urithi huo.
Wakati
wa kongamano hilo washiriki walifanya ziara katika maeneo mbalimbali ya
kitalii kabla ya kufanya majadiliano na kuweka mwelekeo wa namna bora
ya kutengeneza mkakati utakaoshirikisha wadau wote wa utalii katika
eneo hilo.
Alisema
kwa muda mrefu tangu hifadhi hiyo iwe urithi UNESCO na NCAA walikuwa
wakiangalia zaidi suala la hifadhi kiasi cha wananchi kuona kama
wameachwa nyuma hivyo mkakati wa sasa ni kuwawezesha wananchi kufaidi
matunda ya urithi huo kwa kila kada kupewa wajibu wake na kuona namna ya
kuutekeleza ili ndoto iwe kweli.
Mkufunzi ambaye pia ni mtaalamu mshauri wa Unesco, katika masuala ya
utalii endelevu, James Banks akiwaelekeza jambo washiriki wa warsha hiyo
iliyomalizika mwishoni mwa wiki mji mdogo wa Karatu, mkoani Arusha.
“Tumedhamiria
kujenga uwezo… kusaidia wananchi kuongeza kipato chao kutoka kwa
watalii … ukiangalia katika kreta unaweza kuona magari mengi yakiwa na
watalii… tunataka watu wanaoishi katika eneo hili pia wafaidike …”
alisema.
Hifadhi
hii inatambulika duniani kwa kreta yake kubwa, mbuga yenye wanyama
wengi na eneo ambalo inasadikiwa binadamu wa kwanza aliishi kabla ya
kutawanyika duniani
Ikiwa
na ukubwa wa kilomita za mraba 8,300 Hifadhi ya Ngorongoro ndio
hifadhi pekee duniani ambapo wanadamu wanaishi pamoja na wanyama kwa
usalama.
NCA
ilianzishwa mwaka 1971na kutangazwa kuwa urithi wa dunia na UNESCO
mwaka 1979 lakini kwa muda sasa kumekuwepo na mawazo kwamba dhima kubwa
imekuwa kulinda wanyama na mazingira na kusahaua kwamba pale pana
binadamu ambao wanamahitaji na wanataka kufaidika pia na mazingira
ambayo wanayalinda.
Pichani
juu na chini ni washiriki na wadau wa sekta ya utalii kwenye warsha ya
siku nne ya kutengeneza mkakati wa utalii endelevu hifadhi ya Ngorongoro
iliyomalizika mwishoni mwa wiki mji mdogo wa Karatu, mkoani Arusha na
kuandaliwa na Shirika la UNESCO kwa kushirikiana na Ngorongoro
Conservation Area Authority (NCAA).
Kwa mwaka zaidi ya watalii 450,000 huzuru Ngorongoro ikiwa ni asilimia 60 ya watalii wanaofika nchini.
Mtaalamu
mshauri wa Unesco, James Banks, ameelezea kufurahishwa kwake na
kongamano hilo na kusema kwamba linatoa mwanya wa wadau mbali mbali
muhimu Ngorongoro kuona mwelekeo mpya unaostahili kuchukuliwa ili kuwa
na utalii endelevu.
Alisema
matokeo ya mkakati huo sio tu utaongeza mapato serikalini bali pia
utaimarisha utalii kutokana na ushiriki wa moja kwa moja wa jamii
zinazoishi ndani ya hifadhi hiyo.
Mshiriki
mwingine wa kongamano hilo Flora Assey, Afisa Utalii kutoka ofisi ya
Mkuu wa mkoa wa Arusha alielezea kufurahishwa na kongamano hilo hasa kwa
kuchukua mlengo wa masomo kwa vitendo hali ambayo anaamini itabadili
kabisa utekelezaji wa mkakati unaobuniwa kwa sasa.
Naye
Meneja mkuu wa Ngorongoro Serena Safari Lodge, Dismas Simba alielezea
kuridhishwa kwake na kongamano hilo na kusema litawezesha wadau wote
kufanyakazi kwa pamoja kuhakikisha kwamba utalii unakuwa endelevu katika
eneo hilo hasa kwa kuzingatia kwamba eneo hilo ndilo pekee duniani
ambako wanyama na wanadamu wanaishi pamoja.
Naye
Ofisa Mwandamizi wa Miradi na Mratibu wa UNESCO katika masuala ya
urithi wa dunia na utalii endelevu, Peter DeBrine amepongeza hatua
iliyofikiwa na wadau katika kongamano hilo na kusema raundi ya pili Juni
mwaka huu itatoa mwangaza zaidi kwani utarejesha majibu ya maswali
ambayo kila mtu amepewa kuyafanyia kazi.
Alisema
amefurahishwa na kiwango cha kujituma cha wajumbe waliofika katika
kongamano hilo na kusema kwa jinsi ilivyo mabadiliko yanayofikiriwa na
NCAA yatafanikiwa ili wananchi nao wawe wanafaidika moja kwa moja na
uwapo wa urithi huo wa dunia katika maisha yao.
Flora
Assey, Afisa Utalii kutoka ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Arusha akinakili
mambo muhimu wakati wa kuhitimisha warsha hiyo ya siku nne iliyofanyika
katika ukumbi wa mikutano Kudu Lodge and Campsite iliyopo mji mdogo wa
Karatu mkoani Arusha.
Mwenyekiti
wa Baraza la wakina Mama kata ya Oloirobi, Kijiji cha Mokilal mkoani
Arusha, SEKETO OLDUMU akishiriki kwenye kikundi kazi wakati wa warsha ya
siku nne ya kutengeneza mkakati wa utalii endelevu hifadhi ya
Ngorongoro iliyomalizika mwishoni mwa wiki mji mdogo wa Karatu, mkoani
Arusha na kuandaliwa na Shirika la UNESCO kwa kushirikiana na Ngorongoro
Conservation Area Authority (NCAA).
Meneja
Mkuu wa Ngorongoro Crater Lodge | &BEYOND, Markus Schroeder (kulia)
akishiriki kuchangia maoni wakati wa warsha ya siku nne ya kutengeneza
mkakati wa utalii endelevu hifadhi ya Ngorongoro iliyomalizika mwishoni
mwa wiki mji mdogo wa Karatu, mkoani Arusha. Kushoto ni Mkurugenzi Mkazi
wa Shirika la Umoja wa Mataifa la elimu sayansi na utamaduni (UNESCO)
Zulmira Rodrigues.
Kwa matukio zaidi bofya hapa
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
0 comments:
Post a Comment