Home » » Kinapa yamaliza migogoro Longido

Kinapa yamaliza migogoro Longido

MIGOGORO ya wafugaji na wakulima katika Tarafa ya Enduimeti, Wilaya ya Longido, mkoani Arusha imedhibitiwa baada ya Hifadhi ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro (Kinapa), kutoa elimu kwa makundi hayo ikiwamo hifadhi ya mazingira na kuepuka ufugaji wa kuhamahama.
Pamoja na hilo, lakini pia tatizo la baadhi ya wafugaji kutelekeza familia zao kwa kigezo cha kutafuta malisho limemalizika baada ya hifadhi kuanzisha miradi ya kiuchumi kwa lengo la kuwasaidia wafugaji na wakulima.
Ofisa Uhusiano wa hifadhi hiyo, Theodory Lois, alisema hayo wakati akikabidhi mradi wa mbuzi wa maziwa kwa wanawake wa kikundi cha Upendo ambapo pia wamefanikisha maji ya bomba katika Kata ya Kamwanga, ujenzi wa zahanati ya Kijiji cha Irkaswa kuanzisha vikundi vya uzalishaji mali na ufugaji wa kisasa.
“Ile tabia ya kuwapo kwa migogoro ya wafugaji na wakulima sasa itakuwa imekwisha maana hii miradi itawawezesha kukaa eneo moja, kitendo cha kuhamahama kilikuwa kikiwagombanisha na wakulima, tunzeni hii miradi lakini pia otesheni miti ya kutosha,” alisema.
Alisema Kinapa imefanikiwa kudhibiti uharibifu mkubwa wa mazingira katika hifadhi hiyo baada ya wafugaji katika Tarafa ya Enduimeti kusitisha ufugaji wa kuhamahama na kujikita katika fursa za ujasirimali na ufugaji wa kisasa.
Diwani wa Enduimeti, Neema Lee, alipongeza wafugaji kwa kukubali kusitisha utaratibu wa kutafuta malisho kwa kuhamahama kutaibadili jamii hiyo kuwa ya kisasa zaidi.
Chanzo;Tanzania Daima 

0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa