Home » » TUTAHAMA TUKILIPWA FIDIA-MASHAHIDI

TUTAHAMA TUKILIPWA FIDIA-MASHAHIDI

WANANCHI 43 wa vijiji vya Kiding’a, Moivo, Kirevi, Sambasha na Kiranyi, wilayani Arumeru wamesema wapo tayari kupisha ujenzi wa barabara ya Mianzini hadi Timbolo yenye umbali wa kilomita nane endapo watalipwa fidia ya mali walizoendeleza pembezoni mwa barabara hiyo zenye thamani ya zaidi ya sh bilioni 3.2.
Hayo yalielezwa juzi kwa nyakati tofauti na mashahidi watano wa upande wa waleta maombi, mbele ya Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Fatma Mssengi, anayesikiliza shauri la ardhi namba 18/2013 lililofunguliwa na wananchi hao.
Wakiongozwa na wakili wao, Modest Akida, mashahidi hao walidai wako tayari kubomoa nyumba zao na kupisha ujenzi wa barabara hiyo endapo Halmashauri ya Wilaya ya Arusha ambaye ndiye mdaiwa kwenye shauri hilo itawalipa fidia stahiki kwa mujibu ya sheria ya barabara ya mwaka 2007.
Shahidi wa tatu, Gideon Lukumay (74), aliieleza mahakama hiyo kuwa maeneo hayo wanayamiliki kwa mujibu wa sheria za kimila, kwani waliyarithi kutoka kwa mababu.
Alidai anachojua barabara hiyo ni mali ya wananchi, kwani ndiyo wamekuwa wakiikarabati kwa kipindi chote kabla Halmashauri ya Wilaya ya Arusha kuanza kuikarabati.
“Baada ya nyumba zetu kupigwa alama ya  ‘X’ tulipeleka malalamiko halmashauri na kuiuliza kwanini inataka kutubomolea bila kufidiwa lakini hatukupata majibu yanayoeleweka, binafsi ningefidiwa ningeondoka,” alidai Lukumay.
Shahidi wa kwanza, Fanuel Lamai, alieleza kuwa Aprili 14, mwaka jana halmashauri walitumia katapila na kuvunja kingo za barabara, kukata miti kwa kutumia mashine huku zoezi hilo likifanyika chini ya uangalizi wa polisi.
Alielea kuwa hawapingi ujenzi wa barabara hiyo ila wanaomba kulipwa fidia.
Upande wa waleta maombi wamemaliza kutoa ushahidi wao ambapo walileta mashahidi watano, wakiwemo Agnes Martin (67) na Ndeai Nembate.
Katika madai yao ya msingi wananchi hao 43 wanaiomba mahakama hiyo itamke kuwa wao ni wamiliki halali wa ardhi na mali zao zilizopo maeneo ya pembezoni mwa barabara ya Mianzini mpaka Timbolo.
Pia wanaiomba mahakama hiyo iwaelekeze Halmashauri ya Wilaya ya Arusha iwalipe fidia ya ardhi waliyoiendeleza na mali zao yenye thamani ya zaidi ya sh bilioni 3.2, ili waweze kupisha ujenzi wa barabara hiyo ya Mianzini mpaka Timbolo.
Chanzo:Tanzania Dima

0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa