Arusha
Home » » Coaster zaruhusiwa kusafirisha abiria Dar-Kaskazini

Coaster zaruhusiwa kusafirisha abiria Dar-Kaskazini

Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa majini na nchi kavu (Sumatra)
 
Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa majini na nchi kavu  (Sumatra) imeruhusu magari madogo aina ya  Coaster kusafirisha abiria waendao mikoa ya Kaskazini ya Arusha na Kilimanjaro kutoka Ubungo jijini Dar es Salaam ili kupunguza  upungufu wa mabasi kipindi hiki cha sikukuu.
Mkaguzi wa  Sumatra, Masumbuko Masuke, alisema uamuzi huo umefikiwa kwa  lengo la kupunguza  kero kwa wasafiri na  kuboresha huduma.

Alisema kumekuwa na tatizo la baadhi ya abiria kutojua haki zao na wengine kuwahonga makondakta fedha ili kupatiwa tiketi, hivyo kusababisha zoezi la ukaguzi wakati mwingine kuwa mgumu.

“Tunatoa wito kwa abiria wote kuwa makini na kuonyesha ushirikiano  wakati wanapotozwa nauli kubwa au kuuziwa tiketi feki  kwa kutoa taarifa kwenye Mamlaka husika ili wamiliki wa mabasi kufuata sheria kwa kutekelezaji  wajibu wao wa  kutoa huduma stahiki,” alisema.

Msuke alisema abiria  60 walioshindwa kusafiri juzi kutoka Dar es Salaam kwenda mkoani Kagera kwa sababu mbalimbali, lakini walisafirishwa jana na kuwataka wanaotarajia kusafiri kufanya mipango mapema na kampuni za mabasi ili kuepuka utapeli.

Wakati huo huo Sumatra imeyafungia mabasi matatu yanayifanya safari zake katika mikoa ya Arusha, Singida, Manyara na Tanga   kwa muda usiojulikana kuanzia juzi kwa madai ya  kusababisha ajali mara kwa mara.

Mabasi hayo ni Osaka linalokwenda  Arusha, Polepole linalokwenda Singida na Babati, Burudani linalokwenda Korogwe na Lushoto yote  huanzia safari zake kutoka Dar es Salaam.

Wakati huo huo, pamoja na juhudi za  Jeshi la Polisi na Sumatra kukemea kitendo cha mabasi kutoza nauli kubwa, bado mengine wanakiuka agizo hilo.

Baadhi yameongeza nauli kuanzia Sh. 1,000 hadi Sh.5,000 zaidi ya nauli ya awali na kusababisha abiria kulalamikia mamlaka husika kwa kushindwa kuweka adhabu na kusimamia sheria ili kuondoa tatizo hilo.

Mabasi yaliolalamikiwa na abiria ni pamoja na Raha Leo linalokwenda Tanga limeongeza nauli kutoka Sh. 12,000 hadi Sh.13,000, Princess Muro linalokwenda Nzega mkoani Tabora Sh. 39,000 hadi Sh. 40,000 na baadhi ya Coaster zinazokwenda Moshi na Arusha kutoka Sh. 20,000 hadi Sh. 25,000.

Imeandaliwa na Loveness Massero, Kamili Mmbando na Leonce Zimbandu.
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa