Mary Mwita, Arumeru
WANAWAKE wajawazito wilayani Arusha, wametakiwa
kujenga utamaduni wa kuhudhuria vituo vya afya ili waweze kujifungua salama na
kuepuka vifo visivyo vya lazima.
Rai hiyo ilitolewa jana na Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Seif
Selemani Rashid, wakati akizindua jengo la Zahanati ya Oldonyowasi iliyopo
katika Kijiji cha Oldonyowasi, Kata ya Oldonyosambu.
Dk. Rashid alisema ni aibu wajawazito kujifungulia nyumbani, huku akiitaka
jamii kuwa mstari wa mbele kuhamasisha wanawake kupenda kujitokeza na
kuhudhuria kliniki, ili kupata ushauri wa daktari.
Aliwataka wananchi wa Kijiji cha Oldonyowasi kutumia Zahanati iliyojengwa kwa
ushirikiano na wadau wa maendeleo, ikiwamo msaada kutoka Ujerumani.
Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Arusha, Dk Thobias Mkina alisema
kuwa Halmashauri hiyo inakabiliwa na tatizo la ukosefu wa watumishi wa afya na
kuiomba Serikali kupeleka watumishi zaidi.
Mkina alisema halmashauri hiyo imetoa vitanda kwa ajili ya Zahanati ya
Odonyowasi na kueleza kuwa daktari kwa ajili ya zahanati hiyo atapelekwa kwa
jili ya huduma.
Naye Mwenyekiti wa Kitongoji cha Sura Kijiji cha Oldonyowasi, Geofrey Ayo,
aliwashukuru kwa msaada wa kujengewa zahanati hiyo na kufafanua kuwa hali ya
huduma ya afya katika kijiji hicho ilikuwa mbaya kabla ya ujenzi wa zahanati
hiyo.
Ayo alisema zahanati hiyo itasaidia kupunguza kama si kumaliza kabisa tatizo la
vifo vya wajawazito na pia itachochea wananchi kujenga utamaduni wa kwenda
hospitali badala ya kutumia miti shamba
Chanzo: Mtanzania
0 comments:
Post a Comment