Home » » Mahakama ya ICRT kutoa hukumu ya kesi ya Nzabonimana Mei 31, 2012

Mahakama ya ICRT kutoa hukumu ya kesi ya Nzabonimana Mei 31, 2012

Na Woinde Shizza,Arusha

Mahakama ya Kimataifa ya Mauaji ya Kimbari ya Rwanda (ICTR) itatoa hukumu ya kesi inayomhusi Waziri wa zamani wa Vijana wa Rwanda, Callixte Nzabonimana Mei 31, 2012.

Nzabonimana anakabiliwa na mashitaka ya mauaji ya kimbari, kula njama za kufanya mauaji hayo, uchochezi, kuteketeza kizazi na mauaji kama uhalifu dhidi ya binadamu.

Pande zote mbili katika kesi hiyo ziliwasilisha hoja zao za mwisho Oktoba 20 na 21, 2011 huku upande wa mwendesha mashitaka ukitaka impatie adhabu ya kifungo cha maisha jela iwapo mshitakiwa atatiwa hatiani, kwa kuhusika kwake katika mauaji ya kimbari ya mwaka 1994.


Kwa mujibu wa mwendesha mashitaka, Nzabonimana alikuwa mchochezi mkuu wa mauaji hayo mkoani kwake alikozaliwa, Gitarama, katikati ya Rwanda. ‘’Nzabonimana hakuwa Waziri nchini Norway au Sweden bali Waziri nchini Rwanda.Alikuwa kama simba mkoani Gitarama mwaka 1994.Aliweza kusimama na kutoa wito kwa wananchi kuanza kuwaua Watutsi na amri zake zilikuwa zinazingatiwa na kutekelezwa.’’Mwendesha mashitaka, Paul Ng’arua alieleza.



Upande wa utetezi umeiomba mahakama kumwachia huru mteja wao katika mashitaka yote yanayomkabili wakidai kwamba mashitaka hayo ‘’yalitungwa’’ na ‘’yamejaa uongo.’’

Philippe Larochelle, Wakili Msaidizi wa Nzabonimana alidai kwamba mashahidi walioletwa kutoka magerezani nchini Rwanda walikiri kuwa walishawishiwa kuwatuhumu viongozi waliokuwa madarakani wakati wa mauaji ya kimbari ili kupunguziwa adhabu katika hukumu za kesi zao.

Waziri huyo alitiwa mbaroni nchini Tanzania Februari 18, 2008 na kesi yake ilianza Novemba 9, 2009 na kuhitimishwa Septemba 12,2011. Mwendesha mashitaka aliita mashahidi 20 wakati upande wa utetezi uliita mashahidi 38.

0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa