Arusha
Home » » NDESMBURO:CHADEMA ITAINGARAGAZA CCM CHAGUZI ZIJAZO

NDESMBURO:CHADEMA ITAINGARAGAZA CCM CHAGUZI ZIJAZO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Mbunge wa Moshi Mjini, Philemon Ndesamburo.
 
Mbunge wa Moshi Mjini, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), mkoani Kilimanjaro, amesema chama chake kitaendelea kukigaragaza Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika chaguzi zijazo kutokana na kujipanga vilivyo, kuanzia ngazi ya vijiji hadi taifa.
Alisema hayo mjini hapa wakati wa uchaguzi wa kuchagua viongozi wa kamati tendaji ya baraza la vijana la chama hicho mwishoni mwa wiki na kusema bado wapo ‘ngangari’ na wataendelea kushikilia katika ngazi za uongozi kwenye jimbo, vijiji, kata na hata taifa.

Ndesamburo alisema awamu hii hawana mzaha hata kidogo na kwamba, wanaendelea kujiimarisha kisiasa kwa kuwahamasisha vijana wote waliofika umri wa kujiandikisha kupiga kura wanajitokeza kwa wingi na kwamba, watajitokeza katika upigaji kura baadaye mwaka huu.

Alisema Jimbo la Moshi Mjini litaendelea kushikiliwa na Chadema licha ya kuwapo baadhi ya watu kulinyemelea.

Ndesamburo alisema Chadema katu hawatakuwa tayari kuliachia jimbo hilo kutokana na ukweli kwamba, wananchi wake wanahitaji maendeleo na wao (Chadema) ndiyo pekee wenye kutekeleza hayo.

“Leo vijana wanachagua viongozi wao katika baraza lao la vijana. Hawa ndiyo wapiganaji wetu na ndiyo chachu ndani ya chama chetu. Tunawalea ili nao waje wawaletee wananchi maendeleo. Chaguzi zijazo tutaendelea kushika hatamu na lazima tutaongeza majimbo, kata na hata mitaa na vijiji, ambavyo havipo mikononi mwetu,” alisema Ndesamburo.

Hata hivyo, kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Boma Mbuzi, ambaye pia ni Meya wa Manispaa ya Moshi, pamoja na mambo mengine, aliwataka vijana na wanachama wa chama hicho kushirikiana na kushikamana kwa pamoja kutokana na chaguzi zijazo kuwa na upinzani mkubwa tofauti na miaka ya nyuma.

Alisema hali ya kisiasa hivi sasa siyo sawa na ilivyokuwa miaka ya nyuma na kwamba, chaguzi zijazo zitakuwa na changamoto nyingi, hivyo ni vyema kama chama wakashikamana na kuzidi kuweka mizizi imara itakayowawezesha kuibuka na ushindi jambo ambalo anaamini kama Chadema linawezekana.
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa