Arusha
Home » » ZAWADI SOKOINE MIMI MARATHON ZATAJWA

ZAWADI SOKOINE MIMI MARATHON ZATAJWA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
MSHINDI katika mbio za kilomita 10 Sokoine Mini Marathon zinazofanyika Monduli Juu wilayani Monduli mkoani hapa, anatarajiwa kuondoka na kitita cha sh 500,000.
Kwa mujibu wa mratibu wa mbio hizo, Wilhelm Gidabuday, zitahusisha pia walemavu sambamba na michezo mingine ikiwemo ya kuruka chini na kurusha mkuki.
Alisema kuwa kwa upande wa mbio za kilomita 10 zitakazohusisha watu wazima wasio na ulemavu, mshindi wa kwanza atazawadiwa kitita cha sh 500,000, wa pili sh 400,000 huku wa tatu akijipoza na sh 300,000 kwa wanaume na wanawake.
Gidabuday alisema kuwa watakaofanikiwa kushika nafasi ya nne watapata sh 100,000 na wa tano sh 75,000 huku mshindi wa sita akifutwa jasho kwa sh 50,000.
“Hizo ndio zawadi kwa washindi wa mbio ndefu za kilomita 10 kwa mwaka huu, kuanzia wa kwanza hadi wa sita, lakini kwa wale watakaoshindwa hatuna cha kuwapa, zaidi ya kuwatia tu moyo waendelee kukimbia kwa mara nyingine mwakani, kwani wakikazana watashinda huku pia wakitambua kuwa lengo ni kumuenzi aliyekuwa Waziri Mkuu Edward Sokoine,” alisema.
Mbio hizo kwa upande wa walemavu mshindi wa kwanza atajinyakulia sh 200,000 wa pili sh 150,000 huku mshindi wa tatu akiondoka na sh 100,000.
Kuruka chini mshindi wa kwanza atajinyakulia sh 200,000 na wa pili sh 150,000 huku mshindi wa tatu akijipoza kwa sh 100,000 hivyo hivyo katika kurusha mkuki.
Mbio hizo ni sehemu ya matukio yatakayoadhimisha miaka 30 ya kifo cha aliyekuwa Waziri Mkuu wa Tanzania, Edward Moringe Sokoine.
Maadhimisho hayo yatakayoongozwa na Rais Jakaya Kikwete, pia yatahudhuriwa na aliyekuwa Rais wa awamu ya tatu, Benjamini Mkapa na viongozi wengine mbalimbali, ambapo pia kutakuwa na misa maalumu ya kumuombea hayati Sokoine
Kwa mujibu wa Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magessa Mulongo, Rais Kikwete atawasili leo mkoani hapa.
Mbio hizo zitaanza kuanzia saa moja kamili asubuhi na kuisha saa nne, ambapo watu wote watakwenda kanisani kwa ibada maalumu na baadaye rais ataongoza msafara hadi nyumbani kwa familia ya hayati Sokoine, yalipo makaburi na kuweka mashada ya maua.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa