Arusha
Home » » WABUNGE CCM WAVUTANA HOJA BUNGE LA KATIBA KUSIMAMA

WABUNGE CCM WAVUTANA HOJA BUNGE LA KATIBA KUSIMAMA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Mbunge wa Longido CCM), Michael Lekule Laizer
Mbunge wa Longido CCM), Michael Lekule Laizer, na mwenzake wa Viti Maalumu, Dk. Prudenciana Kikwembe, wamevutana kuhusu hoja ya kutaka Bunge Maalumu la Katiba lisimame kwanza hadi hapo mwafaka baina makundi yanayokinzana katika mchakato wa kutunga katiba mpya utakapopatikana.
Mvutano huo uliibuka wakati wa semina kwa wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambao ni wajumbe wa kamati tano za Bunge, juu ya umuhimu wa kusikiliza maoni ya wadau, iliyoandaliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Maendeleo.

Katika maelezo yake, katika semina hiyo, Laizer alishauri Bunge hilo lisimame kwanza na kujikita katika kupata mwafaka baina ya makundi hayo.

Alisema kwa sasa Bunge hilo linaendelea, lakini kukiwa hakuna mwafaka na wengine wakiwa wamesusia mchakato huo na katiba kuonekana ni jambo la vurugu nchini kwa sasa.

“Wananchi ni wadau, kuna viongozi, vyama vya siasa, wataalamu, wasomi, tunaona pamoja na mchango wetu wataalamu na wanasiasa wameipotosha Tanzania, katiba imekuwa kama vurugu, utashi wa kisiasa hadi wananchi wanakosa kujua ukweli ni nini,” alisema.
Aliwaomba wawasilishaji mada kwenye semina hiyo, ambao ni kutoka Bunge la Jamhuri na Mkurugenzi Mtendaji wa Asasi za Kijamii, John Ulanga, kutoa maoni yao iwapo mchakato huo uko katika nafasi nzuri ya kuendelea.
”Kwa kutumia semina hii, kwa sababu hili jambo linaonekana kushindikana, kwa maoni yao wanasemaje, wananchi wanashindwa kuelewa kinachoendelea na msimamo ni upi?” alihoji Laizer.

Hata hivyo, ushauri huo ulipingwa na Dk.Kikwembe akisema kauli ya Laizer kusema wabunge wanashindwa kujadili rasimu ya katiba siyo kweli kwa kuwa wanaendelea kujadili.

”Hatujashindwa kujadili.Tunaendelea kuijadili.Na nina hakika tutafika mwisho. Suala la wenzetu (Ukawa) kutokuwapo ndani sidhani kama kutafanya sisi tushindwe kujadili kwa sababu tunajua ni maoni ya wananchi lazima tujadili,” alisema.

Hata hivyo, Laizer hakuridhika na kauli hiyo na kutaka kupewa nafasi ya kuzungumza zaidi, lakini Mwenyekiti wa semina hiyo, William Ngeleja, aliwasihi wajumbe kutoendelea kuzungumzia suala la katiba ndani ya semina hiyo ya wabunge na siyo wajumbe wa Bunge Maalum.

Alisema mada zinazohusiana na mchakato wa katiba zielekezwe kwenye Bunge Maalumu la Katiba na zipo taratibu za kupeleka maoni.

NUKUU:
“Wananchi ni wadau, kuna viongozi, vyama vya siasa, wataalamu, wasomi, tunaona pamoja na mchango wetu wataalamu na wanasiasa wameipotosha Tanzania, katiba imekuwa kama vurugu, utashi wa kisiasa hadi wananchi wanakosa kujua ukweli ni nini,”
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa