Home » » POLISI ARUSHA YAZIDI KUIMARISHA VIKUNDI VYA ULINZI SHIRIKISHI

POLISI ARUSHA YAZIDI KUIMARISHA VIKUNDI VYA ULINZI SHIRIKISHI




Na Rashid Nchimbi wa Jeshi la Polisi Arusha
Katika kile kinachooneka kuzidi kuhamasisha na kuimarisha Ulinzi na Usalama maeneo mbalimbali ya Mkoa huu, Jeshi la Polisi kupitia Kitengo cha Polisi Jamii mkoani hapa limetoa vizibao 15 kwa kikundi cha Ulinzi Shirikishi cha Muklati kilichopo Ngaramtoni wilayani Arumeru.
Akizungumza wakati wa makabidhiano wa vizibao hivyo leo tarehe 08.01.2014 Adhuhuri, Mkuu wa Kitengo cha Polisi Jamii Mkoa wa Arusha, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi (SSP) Mary Lugola alisema kwamba, Jeshi hilo limeonyesha njia ili kuweza kuwahamasisha wananchi wa maeneo mbalimbali mkoani hapa waweze kuunga mkono juhudi hizo hivyo kujitolea kwa ajili ya kusaidia vikundi hivyo.
Alisema kikundi hicho kilichopo Ngaramtoni kimeweza kuhakikisha eneo hilo linakuwa salama na hali hiyo inatokana na uzalendo walionao vijana hao. Alisema elimu ya ulinzi waliyopata vijana hao imewawezesha kubaini, kuzuia na kupambana na uhalifu hali ambayo imesaidia kupunguza vitendo vya uhalifu na kufanikiwa kukamata silaha mbalimbali zilizotengenezwa kienyeji.

Mkuu huyo wa Polisi Jamii aliendelea kusema kwamba, vizibao hivyo vyenye maandishi ya “ULINZI SHIRIKISHI MKOA WA ARUSHA” vitawasaidia kwenye utendaji wao wa kazi hasa katika suala la utambulisho. Alisema ni vigumu kumtambua mtu au kutambuana mara moja lakini kupitia vizibao hivyo wananchi wa eneo hilo watawatambua kiurahisi na wao kutambuana.

Naye Polisi Tarafa wa eneo hilo ambaye pia Mkuu wa kituo cha Polisi Ngaramtoni, Mkaguzi Msaidizi wa Polisi Elibariki Kileo alizidi kuwasisitiza wananchi wa Tarafa hiyo wajitokeze katika kusaidia kikundi hicho na vingine vilivyopo katika mitaa na vitongoji mbalimbali vya Tarafa hiyo kwani usalama uliopo katika eneo hilo ni matunda ya kikundi hicho.

Aidha kwa upande wake Mwenyekiti wa mtaa wa Muklati Bw. Naima Saitabao alisema kwamba toka kikundi hicho kianzishwe mwaka 2007 hali ya uhalifu imezidi kupungua ikilinganishwa na kipindi cha nyuma. Alisema ushirikiano uliopo kati ya Polisi Tarafa wa eneo hilo, uongozi wake pamoja na wananchi uliwezesha kuanzisha kikundi hicho ambapo kimeweza kudhibiti matukio mengi ya uhalifu kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi.


0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa