Jeshi la Polisi mkoani hapa
limemkamata mtu mmoja aliyejulikana kwa jina la Haji Bakari (25) Mkazi wa Esso
akiwa na kete 58 za madawa ya kulevya yanayodhaniwa kuwa ni Heroine ndani ya
chumba anachoishi.
Akithibitisha kutokea kwa tukio
hilo, Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP)
Ibrahim Kilongo (pichani) alisema kwamba tukio hilo lilitokea tarehe 18/04/2013 muda wa
saa 4:30 usiku maeneo ya Esso jijini hapa.
Kaimu Kamanda Kilongo alisema
kwamba, mafanikio hayo yamepatikana baada ya jeshi la Polisi mkoani hapa kupata
taarifa toka kwa raia wema juu ya kufanyika kwa biashara hiyo ndani ya nyumba
moja iliyopo eneo hilo.
Alisema mara baada ya kupata taarifa hiyo waliifanyia kazi ambapo baaadhi ya
askari waliokuwa doria walikwenda na kufanikiwa kumkamata mtuhumiwa akiwa
kwenye chumba chake pamoja na wenzake 12 ambao walikuwa wakitumia madawa hayo.
“Mara baada ya askari hao
kuingia kwenye chumba cha mtuhumiwa waliziona kete hizo zikiwa
mezani huku watuhumiwa wengine wakiendelea kutumia madawa hayo” Alisema Kaimu
Kamanda Kilongo.
Mpaka hivi sasa tayari
watuhumiwa hao wameshafikishwa mahakamani leo asubuhi mara baada ya upelelezi
wa awali kukamilika ili waweze kujibu tuhuma zinazowakabili.
Hivi karibuni Jeshi la Polisi
mkoani hapa limepata mafanikio makubwa katika ukamataji wa madawa ya kulevya
aina ya mirungi na bangi pamoja na operesheni ya kuteketeza madawa hayo hekari kadhaa yaliyokuwa wilayani
Arumeru iliyofanyika mwanzoni mwa mwezi Machi.
0 comments:
Post a Comment