CHUO CHA VETA ARUSHA CHAZINDUA MRADI WA BIOGAS WENYE THAMANI YA ZAIDI YA SHILINGI MILIONI 150








.....

Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi stadi (VETA) kupitia chuo chake cha VETA Arusha, imezindua Mradi wa kuzalisha Gesi Asilia kwa kutumia Samadi (Biogas), kwa ajili ya matumizi ya wanafunzi na watumishi, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa adhma ya Serikali ya Tanzania ya kuhakikisha matumizi ya nishati safi na endelevu.

Mradi huo wenye thamani ya takribani shilling milioni 156 umezinduliwa rasmi jana, tarehe 12 Februari, 2025, na Profesa Ledislaus Mnyone ambaye ni Mkurugenzi wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, akimwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Prof. Carolyne Nombo.

Mradi huo una uwezo wa kuzalisha gesi asilia kiasi cha 50 cc kwa siku, ambayo ina uwezo wa kutumika kupika chakula cha wanafunzi zaidi ya 400 kwa siku na kutumika katika nyumba sita za walimu pamoja na kantini ya chuo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Profesa Ledislaus Mnyone amesema Mradi huo ni sehemu muhimu ya juhudi za Serikali ya Tanzania katika kufanikisha mpango wake wa kuhakikisha matumizi ya nishati safi na endelevu.

“Serikali imejidhatiti kuimarisha matumizi ya nishati safi inayochangia kupunguza utegemezi wa nishati kutoka vyanzo visivyo endelevu kama vile kuni, mkaa na mafuta” amesema Profesa Mnyone.

Amesema Mradi huo unaenda kuleta manufaa makubwa kwa jamii hasa katika kupunguza uchafuzi wa mazingira na kusaidia katika kutunza rasilimali za asili.

“Nawapongeza sana VETA kwa ubunifu huu, kinachoonekana hapa ni matokeo ya agizo alilolitoa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, ambalo nyie mmelitekeleza kwa vitendo, naomba mradi huu uwe endelevu na kuondokana na ile kasumba mradi ukishazinduliwa haufuatiliwi hadi unakufa. Hii imekuwa ikiipatia Serikali hasara kubwa sana, na sasa tutakuwa tunafuatilia maendeleo ya miradi hii,”amesema.

Aidha ametoa wito kwa taasisi zilizokuwa chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kuhakikisha teknolojia hiyo inasambazwa kote nchini ili kuokoa gharama kubwa ya matumizi ya kuni, lakini pia kuokoa uharibifu wa mazingira.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa VETA nchini, CPA. Anthony Kasore amesema VETA imeanza kutekeleza Mpango wa Serikali katika kuhakikisha matumizi ya nishati safi ya kupikia katika vyuo vyake hasa katika matumizi ya gesi.

“Kupitia mradi huu tunaenda kupunguza gharama za uendeshaji hasa katika kununua kuni, na mkaa, lakini pia tutahakikisha mradi huu unakuwa endelevu na wenye kuleta matokeo,” Amesema CPA. Kasore.

Hata hivyo, CPA. Kasore amesema kwa kupita mradi huu ameona kuna umuhimu wa kuanzisha kozi ya ufugaji, hasa ufugaji wa ng’ombe na ili kupata samadi kwa ajili ya kulisha mtambo huo wa gesi asilia.

CPA Kasore ameishukuru Serikali ya Korea kusini kupitia Wanasayansi na Wahandisi wasio na Mipaka (SEWB) pamoja na Wizara ya Elimu kuwezesha ujenzi wa mradi huo wa BIOGAS.

Aidha Mkurugenzi wa SEWB, Wiin Soo amesema mradi huo ni matokeo ya mazungumzo kati ya ofisi yake na taasisi ya Tume ya Sayansi Teknolojia (COSTECH), ambayo iliomba msaada wa kusaidiwa kujengewa mtambo huo wa mfano ikiwa ni agizo la Mheshimiwa Rais Samia.            

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

MADIWANI KENYA WATEMBELEA TARI TENGERU KUJIFUNZA KILIMO

Madiwani kutoka kaunti ya Eligeyo-Marakwet nchini Kenya wametembelea Kituo cha Utafiti wa Kilimo cha TARI Tengeru kilichopo Arusha kwa lengo la kujifunza shughuli zinazofanywa kituoni hapo ili kuweza kushauri Serikali nchini kwao kutokana na uzoefu wa kazi zinazofanyika nchini Tanzania.

Ugeni huo wa watu 12, ukihusisha madiwani 10, Katibu na dereva ikiwa ni ujumbe wa kamati ya Kilimo, Mifugo, Uvuvi na Umwagiliaji katika kaunti ya Eligeyo-Marakwet, umetembelea TARI Tengeru leo Desemba 02, 2024 ambapo baada ya kupata maelezo ya kazi zinazofanywa na TARI wametembezwa maeneo mbalimbali ya utafiti ili kuona kazi mbalimbali za utafiti zinazofanyika.


Akizungumza kuhusu ujio wa wageni hao, Mkuu wa msafara ambaye ni Mwenyekiti wa kamati hiyo, Mheshimiwa Jeremiah Kibiwott amesema wamechagua kuja kujifunza TARI ikiwa ni Taasisi inayofanya vizuri katika Utafiti wa Kilimo. Amesema ziara hii ni sehemu ya utaratibu wao kujifunza katika Taasisi zinazofanya vizuri za ndani na nje ya nchi ya Kenya TARI ikiwa ni Miongoni.

Mheshimiwa Kibiwott ameendelea kusema, ujio wao Tanzania hususani TARI ni kutokana na kuwa na kiu ya kufahamu tafiti zinazofanyika kwani mazingira na hali ya hewa ya Arusha na eneo wanalotoka inafanana sana hivyo wanaamini matokeo ya utafiti wa TARI Tengeru Tanzania yanaweza kufaa katika maeneo yao nchini Kenya.

Mheshimiwa Kibiwott ameeleza kufurahishwa namna TARI Tengeru inavyofanya Tafiti ambazo zinajibu changamoto za Kilimo na kusema ziara hiyo ni mwanzo wa kuwepo programu za Wataalamu wa pande mbili kubadilishana ujuzi na uzoefu ili kusaidia zaidi Wakulima.

Akitoa wasilisho kwa wageni hao Mkurugenzi Idara ya Uhaulishaji wa Teknolojia na Mahusiano TARI Dkt Sophia Kashenge amesema TARI kupitia mtandao wake wa vituo 17 nchini inafanya tafiti mbalimbali zinazolenga kuleta tija katika mnyororo mzima wa thamani wa mazao mbalimbali

Dkt. Sophia amesema ikiwa suala la uzalishaji tija halitazingatiwa athari zake ni uwepo wa njaa hasa wakati huu bara la Afrika linapotajwa kuwa na ongezeko kibwa la Watu.

Kwa upande wake, Meneja wa Kituo cha TARI Tengeru Dkt. Happy Mollel amewapongeza madiwani hao kutembelea TARI Tengeru ambapo amesema wamepata kujifunza shughuli mbalimbali zinazotekelezwa katika kituo hicho chenye dhamana ya Utafiti wa Mazao ya Bustani.

Aidha Dkt. Happy amewaeleza wageni hao dhamira ya TARI Tengeru kuendelea kufanya tafiti mbalimbali zinazolenga kuleta tija na kusema kuwa kwasasa kituo kipo hatua za mwisho kutoa aina 19 mpya za mbegu bora za Mazao ya Bustani
 

Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam Bi. Tabu Shaibu aliyemwakilisha Mkurugenzi Jiji la Dar es Salaam Elihuruma Mabelya, akipata maelezo kuhusu Mbegu  bora aina 19 za TARI Tengeru ambazo ziko hatua ya mwisho za usajili ili kwenda kwa Wakulima.

 

Mkurugenzi idara ya Uhaulishaji wa Teknolojia na Mahusiano TARI Dkt Sophia Kashenge akitoa wasilisho kwa wadau wa Kilimo cha mbogamboga katika mnyororo mzima wa thamani katika Mkutano uliofanyika Leo Desemba 04, Dar es Salaam
 

Baadhi ya wadau wa mboga mboga katika kuongeza  mnyororo wa thamani wakisikiliza mada mbalimbali.



Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

WAZIRI JAFO ASHIRIKI MKUTANO WA 46 WA BARAZA LA MAWAZIRI EAC


 Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Dkt. Selemani Jafo (Mb.) akiwa na Mawaziri wenzake ameshiriki Mkutano wa 46 wa Kawaida wa Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) unaofanyika Makao Makuu ya Afrika Mashariki Novemba 28, 2024 jijini Arusha.

Waziri Jafo ameshiriki Mkutano huo kwa mara ya kwanza tangu kuteuliwa kwenye wadhifa huo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan mwezi Julai 2024, ameungana na Mawaziri wenzake wanaosimamia masuala ya Afrika Mashariki na Ushirikiano wa Kikanda katika Jumuiya hiyo kupitia, kujadili na kupitisha mapendekezo ya agenda mbalimbali zinazolenga kuboresha utendaji wa Jumuiya kwa manufaa ya Nchi Wanachama ambazo zitawasilishwa kwenye Mkutano wa 24 wa Wakuu wa Nchi wa Jumuiya unaotarajiwa kufanyika tarehe 29 na 30 Novemba 2024 kwa ajili ya kuridhiwa.

Awali akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano huo, Mwenyekiti kutoka Jamhuri ya Sudan Kusini ambaye pia ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Deng Alor Kuol amewapongeza Mawaziri kwa kushiriki mkutano huo na kuwaomba kutoa michango yao chanya katika agenda zilizowasilishwa kwao kabla ya kuziwasilisha kwenye Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa Jumuiya hiyo utakaofanyika tarehe 29 na 30 Novemba 2024.

Miongoni mwa agenda zilizojadiliwa na kupitishwa na Baraza hilo ni pamoja na ripoti ya utekelezaji wa maazimio mbalimbali yaliyofikiwa na Baraza hilo kwenye vikao vilivyopita; taarifa kutoka Ofisi ya Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, taarifa ya utekelezaji wa program mbalimbali katika sekta za miundombinu, forodha na biashara, utalii na ajira; taarifa ya mwaka ya ukaguzi wa hesabu za jumuiya kuanzia mwezi Januari hadi Juni 2024 na ripoti ya kamati ya utawala na fedha, pamoja na kupitia na kupitisha ratiba ya shughuli za Jumuiya kwa kipindi cha kuanzia mwezi Januari hadi Juni 2025.

Ujumbe wa Tanzania katika Mkutano huo umeongozwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.) na umejumuisha Mawaziri wengine Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo, Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi.

Ujumbe wa Tanzania pia uliwajumuisha Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki Balozi Stephen Mbundi, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Samuel Shelukindo, Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Dkt. Tausi Kida, Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha, Mhe. Elijah Mwandumbya, Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-Zanzibar, Kazi, Uchumi na Uwekezaji, Bw. Rashid Ali Salim na Maafisa Waandamizi kutoka Serikalini.

Miongoni mwa majukumu ya Baraza la Mawaziri la Jumuiya ni kutunga sera za Jumuiya, kufuatilia na kufanya mapitio ya mara kwa mara juu ya utekelezaji wa program mbalimbali za Jumuiya kwa maslahi mapana ya Nchi Wanachama.

Jumuiya ya Afrika Mashariki ambayo inaundwa na nchi nane za Tanzania, Kenya, Uganda, Burundi, Rwanda, Sudan Kusini, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Somalia imeendelea kuhakikisha wananchi katika nchi hizo wananufaika na Mtangamano huo hususan katika nyanja za biashara, ulinzi na usalama, viwanda, kilimo, miundombinu na huduma za kijamii.   

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

RAIS SAMIA ATUNUKU KAMISHENI KWA MAAFISA WANAFUNZI 236


Na Pamela Mollel,Arusha

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Samia Suluhu Hassan,ametunuku kamisheni kwa Maafisa Wanafunzi 236 cheo cha luteni Usu,kwa kundi la 05/21-shahada ya Sayansi ya kijeshi(BMS)na kundi la 71/23-Regular katika chuo cha Mafunzo ya kijeshi Monduli leo tarehe 28 Novemba 2024

Aidha kati ya wahitumu hao wanaume 196 na wanawake 40

Maafisa hao wapya wamekuwa Maafisa wa jeshi la Ulinzi la wananchi wa Tanzania (JWTZ)Katika cheo cha Luteni Usu ambapo kundi la 05/21-BMS lenye idadi ya 75 wamepata mafunzo kwa muda wa miaka mitatu na kuhitimu shahada ya Sayansi ya kijeshi

Aidha kundi la 71/23-Regular lenye idadi ya 95 Maafisa wapya wamepata mafunzo yao kwa muda wa mwaka mmoja na Maafisa wengine wapya 88 wamepata mafunzo yao kutoka nchi rafiki za Afrika na nje ya Bara la Afrika

Hata hivyo Kabla ya kutunuku kamisheni Mhe. Rais na Amiri Jeshi Mkuu alikagua gwaride lililoandaliwa na Maafisa Wanafunzi kutokana na maelekezo ya Mkuu wa chuo cha Mafunzo ya kijeshi Monduli,Meja Jenerali Jackson Jairos Mwaseba na kusimamiwa na Kaimu mkufunzi Mkuu Kanali Ally Mohamed Ninga na Kisha kutoa zawadi kwa Maafisa Wanafunzi waliofanya vizuri

Baada ya kamisheni Mhe, Rais alitunuku shahada ya Sayansi ya kijeshi kwa Maafisa wapya 75 pamoja na kuvunja mahafali hayo

Akizungumza katika mahafali hayo ya tano ya shahada ya kwanza Sayansi ya kijeshi,Mkuu wa chuo cha Mafunzo ya kijeshi Monduli Meja Jenerali Jackson Jairos Mwaseba anasema chuo hicho kinaona fahari kubwa kwani hii ni mara ya pili kuwezesha mafunzo ya shahada hiyo kwa kujisimamia pasipo na ushirikiano wa kimafunzo na chuo cha Uhasibu Arusha

Sherehe za kamisheni na mahafali zimehudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali na kijeshi.





Matukio mbalimbali wakati wa sherehe za kutunuku Kamisheni kwa Maafisa Wanafunzi 236 wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania katika sherehe zilizofanyika katika Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi (TMA) Monduli mkoani Arusha tarehe 28 Novemba, 2024













 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa amesimama wakati Wimbo wa Taifa ukiimbwa mara baada ya kuwasili katika viwanja vya Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi (TMA) Monduli mkoani Arusha tarehe 28 Novemba, 2024.



Maafisa wanafunzi wakivalishana vyeo mara baada ya kutunukiwa Kamisheni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Mhe. Samia Suluhu Hassan katika sherehe zilizofanyika kwenye Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi (TMA) Monduli mkoani Arusha tarehe 28 Novemba, 2024


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwatunuku Kamisheni Maafisa Wanafunzi 236 wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania katika sherehe zilizofanyika katika Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi (TMA) Monduli mkoani Arusha tarehe 28 Novemba, 2024


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Mhe. Samia Suluhu Hassan akikagua Gwaride la Heshima kabla ya kutunuku Kamisheni Maafisa wanafunzi 236 wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania katika sherehe zilizofanyika katika Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi (TMA) Monduli mkoani Arusha tarehe 28 Novemba, 2024

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

WAKILI MKUU WA SERIKALI AKUTANA NA RAIS WA MAHAKAMA YA JUMUIYA YA AFRIKA MASHARIKI JIJINI ARUSHA


Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi (kushoto) akimkabidhi zawadi ya Jarida la Ofisi ya Wakili Mkuu Rais wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki baada ya kikao baina yao kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Mahakama hiyo Jijini Arusha.
Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi (kushoto) akipokea zawadi kutoka Rais wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Mhe. Jaji Nestory Kayobera baada ya kikao baina yao kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Mahakama hiyo Jijini Arusha.
Wakili MKuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi (wa pili kushoto) na ujumbe wake wakisikiliza wasilisho kuhusu Mahakama ya Jumjuiya ya Afrika Mashariki inavyofanyakazi alipotembelea Mahakama hiyo Jijini Arusha.
Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi (wa pili kulia) akiwa na viongozi wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki alipotembelea moja ya ukumbi wa Mahakama hiyo baada ya kikao baina yao kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Mahakama hiyo Jijini Arusha.
Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi (wa kwanza kulia) akiwa kwenye picha ya pamoja na Rais wa Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Mhe. Jaji Nestory Kayobera (aliyesimama katikati), Jaji Kiongozi wa Mahakama hiyo, Mhe. Yohane Masara na watumishi wengine baada ya kikao baina yao kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Mahakama hiyo Jijini Arusha.
Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi akiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali na Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki baada ya kutembelea Mahakama hiyo kwa lengo la kuona namna inavyotekeleza majukumu yake jijini Arusha.
Jaji kiongozi wa Mahakama ya Jumuiya ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Mhe. Jaji Yohane Masara akizungumza wa Viongozi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali na Mahakama hiyo wakati wa ziara ya Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi alipotembelea Mahakama hiyo kwa lengo la kujionea jinsi Mahakama hiyo inavyotekeleza makujumu yake jijini Arusha.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa