Arusha
Home » » Askofu: Tanzania ijihadhari na ugaidi

Askofu: Tanzania ijihadhari na ugaidi



ASKOFU John Lenkishon Kispan wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri nchini Kenya (ELCK), ameishauri Serikali ya Tanzania kuchukua tahadhari juu ya matukio ya ugaidi kwa kuimarisha ulinzi katika mipaka yake hasa ule wa Namanga na kutumia mashine maalumu za kukagua wageni wanaoingia na kutoka.

Askofu Kispan alitoa wito huo jana kwenye mpaka wa Tanzania na Kenya alipokutana na Askofu Solom Masangwa wa kanisa hilo nchini, Dayosisi ya Kaskazini Kati, katika ibada ya usharika wa Namanga, wilayani Longido.

Akizungumza baada ya kumalizika kwa ibada hiyo, Askofu Kispan alisema matukio ya ugaidi yanaitesa Kenya kutokana na magaidi kuwaua watu wasio na hatia.

"Nashauri zitumike mashine maalumu za kufanya ukaguzi katika mipaka yenu ili kuwabaini magaidi na kukagua hati za kusafiria, wakati tulionao si wa kumuamini kila mtu kwani leo anaweza kuwa mtu mwema na kesho akawa adui," alisema.

Kwa upande wake, Askofu Masangwa alisema kutokana na matukio hayo nchini Kenya, Serikali ya Tanzania imeanza kuchukua tahadhari na kanisa limeanza kuimarisha ulinzi kwenye nyumba za ibada zilizopo mipakani katika ibada.

Alitoa pole kwa Serikali ya Kenya kutokana na tukio la ugaidi lililowakuta hivi karibuni na kusababisha watu 148 kupoteza maisha katika Chuo Kikuu cha Garissa.

Mkuu wa Jimbo la Arusha Magharibi, Mchungaji Isaac Kissiri, alisema tukio hilo ni la kinyama na linapaswa kulaaniwa na watu wote wapenda amani.

Ili kuonesha ushirikiano uliopo kwa kanisa hilo upande wa Kenya na Tanzania, Maaskofu hao, wachungaji, waumini na
wanakwaya walipanda miti 50 iliyotolewa na Halmashauri ya Longido katika eneo la Kanisa ili kutunza mazingira

 

Chanzao Gazeti la Mwananchi



Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa