Arusha
Home » » LUKUVI AFYATUKA,ARUSHA KOMBORA CUF

LUKUVI AFYATUKA,ARUSHA KOMBORA CUF

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 


Naye Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi jana aliwatolea uvivu viongozi wa UKAWA kutokana na kulazimisha hoja zao ili kupata fursa ya kuongoza dola.

Pia alifichua siri kuwa viongozi wa CUF na CHADEMA wameungana kwa mkataba wa kila upande kuunda serikali na ndio sababu wanashupalia serikali tatu licha ya kuwa na changamoto lukuki.
Alikituhumu CUF kuendesha siasa zake kupitia kivuli cha kikundi cha Uamsho, jambo ambalo ni hatari kwa mustakabali wa taifa.
Lukuvi alitoa kauli hiyo baada ya kupewa nafasi ya kujibu tuhuma zilizoibuliwa na Profesa Lipumba kuwa alitumia sherehe za kumsimika Askofu wa Kanisa la Methodist la mjini hapa, kupigia chapuo muundo wa serikali mbili na kutoa vitisho kuhusu serikali tatu.
Alisema Uamsho wamekuwa wakiendesha siasa za CUF kwa kupitia kivuli cha dini, hivyo hakuna shaka kuwa hata kitakapopata madaraka ,utawala wake utakuwa wa kidini.
“Mambo mengi wanayoyasema wanachama wa CUF ndiyo yanayosemwa na taasisi hiyo, hivyo kwa hofu yangu binafsi, sina shaka Uamsho ni CUF kwani hata Wazanzibar wenyewe wanajua hilo,’’ alisema.
‘’ Hatujawahi kuona Chama kinachojitayarisha kuchukua madaraka kinatumia mgongo wa dini kufanya siasa. Hii si sahihi, kwanini nisiwe na hofu na kusema,’’ alisisitiza
Akizungumzia Jeshi kuchukua madaraka, Lukuvi alisema hofu yake hiyo imetokana na rasimu ya katiba, ambayo inapendekeza kuwepo kwa serikali tatu, jambo ambalo serikali moja ya Muungano vyanzo vyake vya mapato havikuwekwa wazi.
“Haya yalikuwa ni mawazo yangu binafsi na sikuwa na shida kuyaeleza na nitaendelea kuyaeleza na kisiwe chanzo cha wanachama wa UKAWA kudai kuwa hiyo ni lugha ya uchochezi.
“Hivi kati ya mimi na Maalim Seif (Katibu Mkuu wa CUF) nani ni mchochezi ? Mbona hawakugomea kauli yake aliyoitoa Kibanda Maiti kuwa Rais Kikwete atamtuma Mkuu wa Majeshi Mwamunyange kwenda kupindua nchi iwapo serikali tatu zitapita,’’ alisema lukuvi.
Aliwataka wajumbe wa Bunge hilo kufanya kazi waliyokabidhiwa ya kupitia rasimu iliyopendekezwa na si kutafuta visingizio kama inavyofanya UKAWA.
Juzi, Profesa Lipumba alisema Lukuvi alisikika akisema kuwa endapo serikali tatu zitapita, jeshi litachukua nchi.
Akizungumza jana asubuhi, Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samwel Sitta alisema, wamelazimika kumuita Lukuvi ndani ya bunge ili aweze kutoa maelezo kuhusiana na kauli yake iliyodaiwa na Lipumba kuwa ni chanzo cha kususia bunge.
Alisema awali Lukuvi alitakiwa kusafiri kwenda nchini India kwa matibabu, lakini amemrudisha ili kutoa ufafanuzi wa tuhuma hizo kwanza.
Sitta alisema jambo la wajumbe hao wa UWAKA la kususia Bunge kwa madai ya kauli za uchochezi halikustahili kufanywa kwani, kila kero ina utaratibu wake wa kushughulikiwa.
Alisema kuteuliwa na Rais kuwa miongoni mwa watunga katiba ni jambo la heshima na ya kipekee kwani utungaji wa katiba si jambo ambalo hufanyika kila mara.
“Baadhi ya wajumbe wenzetu hawajatambua uzito wa jambo hilo, kwani wakati wote kumekuwa na mambo kadhaa hapa ndani, lakini yamevumiliwa kwa nia njema ili tufikie mwisho ulio salama,”alisema.
Makamu Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samia Suluhu Hassan, alisema kitendo kilichofanywa na wajumbe wa UKAWA hakiwatendei haki Watanzania.
Pia,alisema watakutana na Kamati ya Uongozi  kujadiliana hatua zaidi za kuchukua.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa