Arusha
Home » » Wataka wanawake waruhusiwe kuchumbia

Wataka wanawake waruhusiwe kuchumbia


MKAZI wa Wilaya ya Arumeru, mkoani Arusha, Phillipo Tango (25), amependekeza Katiba Mpya itoe haki na usawa katika suala la ndoa kwa wanawake kuruhusiwa kuchumbia, kutoa mahari na kuoa wanaume wanaowapenda na kukubaliana.
Akitoa maoni yake mbele ya Wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mpya juzi, Tango ambaye ni mkazi wa Kata ya Olmotonyi, wilayani Arumeru alisema lazima Katiba hiyo mpya ikomeshe mfumo dume unaotawala suala la ndoa.
“Katiba itoe haki sawa kwa jinsi zote mbili katika suala la kuoana na haki zote za ndoa tofauti na sasa ambapo wanaume ndiyo wenye maamuzi makubwa kulinganisha na wanawake,” alisema Tango.
Kwa upande wake, Makamba Meshilieki (32), mkazi wa kijiji cha Ngaramtoni yeye alipendekeza wabunge na madiwani kuingia mikataba na wananchi wa maeneo yao kuhusu utendaji na utekelezaji wa miradi ya maendeleo mara baada ya kushinda uchaguzi.
Alipendekeza pamoja na kuonyesha muda wa utekelezaji, mkataba baina ya wabunge, madiwani na wananchi kutaja adhabu atakayostahili kiongozi anayeshindwa kutimiza wajibu wake kwa jamii.
“Mbunge au diwani atakayeshindwa kutimiza yaliyoahidi katika mkataba wachapwe viboko 60 hadharani ili kuwa fundisho kwa wengine wenye tabia ya kutoa ahadi zisizotekelezeka kipindi cha kampeni za uchaguzi,” alisema Tango.
Emanuel Mollel (44), yeye alitaka Katiba Mpya kuwazuia viongozi na watendaji Serikalini, mashirika na taasisi za Umma kufanya biashara wakiwa madarakani ili kudhibiti migongano wa kimaslahi.
Alisema viongozi kuendelea kushiriki shughuli za kibiashara wakiwa madarakani kunachochea vitendo vya ubadhirifu, wizi na matumizi mabaya ya madaraka na ofisi za umma kwa faida na maslahi binafsi.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa