Arusha
Home » » SHAHIDI AELEZA DOLA ZILIVYOKWAPULIWA BENKI EXIM ARUSHA.

SHAHIDI AELEZA DOLA ZILIVYOKWAPULIWA BENKI EXIM ARUSHA.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

Imeandikwa na John Mhala, Arusha
Jengo la Mahakama Kuu.
KESI ya wizi ya Sh bilioni saba inayowakabili waliokuwa wafanyakazi 14 wa benki ya Exim ya jijini Arusha, iliendelea kusikilizwa juzi na jana. Shahidi wa pili katika kesi hiyo, Raymond Matiko (35) aliieleza Mahakama kuwa miamala ya fedha za kigeni (dola), ilichukuliwa kutoka katika akaunti sita zilizofunguliwa katika benki hiyo.
Matiko ambaye wakati huo wa wizi alikuwa Meneja wa Operesheni makao makuu ya benki hiyo jijini Dar es Salaam na pia Mkuu wa Kitengo cha Mfumo wa Kielektroniki katika benki hiyo, alisema kuwa mfumo wa kisasa wa elektroniki, ulianza katika benki hiyo mwaka 2010.
Shahidi huyo alikuwa akitoa ushahidi wake, akiongozwa na Mwanasheria wa Serikali, Paul Kaduchi. Alidai kuwa akaunti hizo sita, zilifunguliwa na wateja na zilitumika kukwapua miamala ya dola kutoka katika kampuni mbalimbali za kitalii na watu binafsi waliokuwa wakiweka pesa katika benki hiyo.
Alitaja akaunti na majina ya akaunti kuwa ni akaunti namba 5701555011 ya Nuru Benedicti Sanga, 0031023792 ya Mosses Chacha Aloyce, 0031023771 ya Gervas Fulgence Kimaro, 5795276654 ya Furahini Elibariki Ngoda, 5795340108 ya Tumaini Raphael Mwandingo na 0031023088 ya Raymond Allais Telekish.
Alidai mbele ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Arusha/Arumeru, John Kamugisha kuwa fedha hizo ziliingizwa na kuidhinishwa na baadhi ya watuhumiwa katika akaunti hizo. Shahidi huyo alitoa kielelezo P2 ambacho ni akaunti ya dola, iliyokuwa ikionesha jinsi maelfu ya dola yalivyokuwa yakiingizwa, kuidhinishwa na kuhamishwa kutoka akaunti za kampuni mbalimbali za kitalii na binafsi jijini Arusha na watuhumiwa hao.
Hata hivyo, kielelezo hicho kilipingwa vikali kupokelewa na mawakili wa watuhumiwa kwa kuwa hakikuidhinishwa na wakili, kama ni nyaraka halali ya benki pamoja na kuwa na mhuri wa benki. Lakini, mwanasheria wa serikali, Kadushi alijenga hoja ya kutaka Mahakama kukubali kielelezo hicho kipokelewe mahakamani hapo na hakimu alikikubali.
Matiko alitaja baadhi ya kampuni za kitalii, zilizochotewa fedha zao ni Kibo, Leopard, Ranger Safari na Bushback na kampuni nyingine za watu binafsi. Shahidi huyo alidai walioidhinisha kuingiza maelfu ya dola katika kaunti hizo maalumu ni watuhumiwa hao hao ; na walioidhinisha kutoka ni watuhumiwa hao pia.
Katika kesi hiyo, wafanyakazi 14 na mfanyabiashara mmoja wanatuhumiwa kuiba zaidi ya Sh bilioni saba kwa kughushi, utakatishaji fedha na wizi wa mfumo wa kibenki kwa nyakati tofauti mwaka 2011 hadi 2012.
Wafanyakazi hao ni aliyekuwa Meneja wa Benki Tawi la Exim Arusha, Bimel Gondalia (37), Lilian Mgaya (33), Neema Kinabo (30), Livingstone Julius (36), Joyce Kimaro (36), Daud Mosha, Doroth Tigana (50) na Evans Kashebo (40).
Wengine ni Mosses Chacha (37), Tuntufe Agrey (32), Joseph Meck (34), Janes Massawe (32), Christophe Lyimo (34), Deodet Chacha (35) na Gervas Gugo ambaye ni mfanyabiashara. Washitakiwa wanne ambao ni Gomes, Kashebo, Neck na Lyimo, wapo nje kwa dhamana.
CHANZO: HABARI LEO.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa