Arusha
Home » » JUHUDI BINAFSI ZINATAKIWA KUMALIZA UKEKETAJI, UNYANYASAJI KIJINSIA – ROSE HAJI MWALIMU‏

JUHUDI BINAFSI ZINATAKIWA KUMALIZA UKEKETAJI, UNYANYASAJI KIJINSIA – ROSE HAJI MWALIMU‏

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

IMG_1260
Afisa Maendeleo ya Jamii (W) Ngorongoro, Teresia Irafay (wa pili kushoto) akiitambulisha meza kuu kabla ya kumkaribisha Katibu Tawala wa Wilaya ya Ngorongoro, Lemuel Kileo, (wa tatu kulia) kufungua kongamano la viongozi wa mila wa kabila la wamasai (Laigwanan/Ngaigwanani) na wanawake Mashuhuri yenye lengo la kushawishi uondoaji wa mila potofu zinazorudisha nyuma maendeleo katika jamii za wafugaji. Kushoto ni Mtaalamu wa masuala ya vyombo vya habari vya kijamii na Mkufunzi kutoka (UNESCO), Bi. Rose Haji Mwalimu, Kiongozi wa Malaiboni wilaya ya Ngorongoro Bw. Sangau Naimodu (wa pili kulia) pamoja na Katibu wa Baraza Mila (W) Ngorongoro, Laanoi Munge, (kulia), Mwenyekiti wa Baraza la Malaigwanan wilaya ya Ngorongoro, Joseph Oletiripai (wa tatu kushoto). (Picha zote na Zainul Mzige wa Modewjiblog).
Na Modewjiblog team
JAMII ya wafugaji imetakiwa kutumia juhudi zao binafsi kubadilisha mawazo na imani ya jamii kwamba mila na desturi hazibadiliki ili kutengeneza mfumo bora mpya unaothamini maisha ya wanawake.
Wito huo umetolewa na Mtaalamu wa masuala ya vyombo vya habari vya kijamii na Mkufunzi, Bi. Rose Haji Mwalimu wakati akiwasilisha mada kwenye kongamano la viongozi wa mila wa kabila la wamasai (Laigwanan/Ngaigwanan), Laiboni na wanawake Mashuhuri yenye lengo la kushawishi uondoaji wa mila potofu zinazorudisha nyuma maendeleo katika jamii za wafugaji.
Aliwataka washiriki wa warsha kusimama kidete na kutumia elimu waliyoipata katika kushawishi jamii kubadilika na kuachana na mila za ukekeketaji,ndoa za utotoni na pia unyanyasaji mwingine wa kijinsia unaoonesha ubabe wa wanaume na mfumo dume.
Aliwataka wanajamii hao kutumia njia mbalimbali ikiwemo vyombo vya habari, rediojamii, vikao mbalimbali vya kata na vijiji pamoja na nyumba za ibada kuhimiza watu kubadilika na kuacha mila hizo za ukeketaji na kuozesha watoto katika umri mdogo.
Aidha Bi. Rose Haji Mwalimu katika kongamano hilo lililoandaliwa na Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni la Umoja wa Mataifa, (UNESCO) amewataka wanawake kuvunja ukimya na kuacha uoga na kuibua vitu vinavyowanyima haki zao za msingi.
IMG_1277
KatibuTawala wa Wilaya ya Ngorongoro, Lemuel Kileo akifungua kongamano la viongozi wa mila (Laigwanan/Ngaigwanan na Laibon) pamoja wanawake mashuhuri lenye lengo la kuondoa mila potofu zinazokwamisha maendeleo katika jamii za wafugaji ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya wilaya ya Ngorongoro.
Aliwataka wanawake kujitambua ili kutumia sheria zinazowalinda kuondokana na unyanyasaji pamoja na ukatili wa kijinsia unaoendelea katika jamii za kifugaji na kuwaomba viongozi wa mila washiriki katika kuondoa mfumo dume.
Naye Ofisa Ustawi wa Jamii wa halmashauri ya wilaya ya Ngorongoro, Benezeth Bwikizo, amesema kama watuw atajitokeza na kueleza ukweli serikali itachukua hatua hasa ya kulinda wanawake na watoto kupitia mamlaka iliyokabidhiwa na Katiba ya nchi.
Alisema kwa mujibu wa sheria Serikali ina mamlaka ya kuhakikisha kwamba haki za watoto zinalindwa kupitia sheria ya mtoto namba 21 ya mwaka 2009 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwamba mtoto lazima alindwe na apate haki zake zote za msingi.
Alisema pamoja na katika na sheria zilizotungwa, mtoto pia analindwa na mkataba wa kimataifa wa haki za mtoto wa Novemba 20, 1989 inayotoa ufafanuzi wa kulinda na kuhakikisha kwamba haki za mtoto zinalindwa na kuheshimiwa.
Aliongeza kuwa pia ulindaji huo wa haki za mtoto unakwenda sanjari na mkataba wa Umoja wa nchi za Afrika ya mwaka 1990 unaotoa ufafanuzi juu ya haki za msingi za mtoto na namna inavyotakiwa kuheshimiwa na kulindwa bila kuathiri haki zao.
IMG_1323
Ofisa Elimu ya Uzazi na UKIMWI kutoka UNESCO, Mathias Herman akizungumzia malengo ya kongamano hilo kwa washiriki.
Bw.Bwikizo, alitaja haki za muhimu kwa mtoto zinazotakiwa kulindwa na kuheshimiwa ili kuhakikisha mtoto anakua katika malezi bora ni huduma za afya, chanjo, matibabu, Lishe na malezi bora kupata haki ya kuishi, haki ya kuendelezwa na haki ya kulindwa.
Akizungumza katika ufunguzi wa kongamano hilo, KatibuTawala wa Wilaya ya Ngorongoro, Lemuel Kileo, amelishukuru Shirika la UNESCO kwa kuendesha mafunzo hayo ya kutoa elimu na kujenga uwezo kwa viongozi wa mila na wanawake mashuhuri ili kuondoa mila potofu katika jamii ikiwemo Ukeketaji, mimba za Utotoni na ndoa za umri mdogo.
Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya, Bw. Kileo aliwataka viongozi na washiriki wa warsha hiyo watumie nafasi hiyo waliyoipata kwenda kufikisha ujumbe kwa jamii ili kupeleka maendeleo mbele kwa kupunguza vifo vya akinamama na wasichana wenye umri mdogo, kuondokana na ukeketaji pamoja na mimba za umri mdogo.
IMG_1338
Mtaalamu wa masuala ya vyombo vya habari vya kijamii na Mkufunzi kutoka UNESCO, Bi. Rose Haji Mwalimu akisisitiza jambo kwa washiriki wa kongamano.
Kwa upande wa mmoja wa wakufunzi wa warsha hiyo kutoka UNESCO akizungumzia malengo ya warsha hiyo, Ofisa Elimu ya Uzazi na Ukimwi wa shirika hilo, Mathias Herman, amesema warsha hiyo ni mwendelezo wa warsha zinazotolewa na UNESCO kwa ajili ya kutoa elimu ya kuwajengea uwezo na kugawa majukumu kwa viongozi wa kimila (Laigwanan), wa mama mashuhuri, viongozi wadini, wakunga wa jadi pamoja na waandishi wa habari kufanya ufuatiliaji wa afya ya uzazi na malezi bora kwa watoto.
Aliongeza kuwa UNESCO inatarajia mafunzo hayo kutaleta mabadiliko kupitia nafasi ya viongozi hao mashuhuri katika jamii kwa kuwa wanaaminika ili kushirikiana na wadau wengine wa maendeleo wanaotoa mafunzo kuhakikisha kwamba suala la mimba za utotoni, ndoa za utotoni pamoja na ukeketaji linafika mwisho katika jamiii ya kifugaji.
IMG_1421
IMG_1269
Mwenyekiti wa Baraza la Malaigwanan wilaya ya Ngorongoro, Joseph Oletiripai akisisitiza jambo kwa Malaigwanan pamoja na wakina mama mashuhuri ambapo aliwataka watumie nafasi waliyopewa na jamii na fursa ya elimu waliyopata kutoka kwa wadau wa maendeleo UNESCO kuwa italeta mabadiliko na mpango chanya katika jamii ya Kimasai.
IMG_1443
Ofisa Ustawi wa Jamii wa wilaya ya Ngorongoro, Benezeth Bwikizo (kuhoto) akizungumzia haki za watoto. Kulia ni Mkalimani wa lugha ya Kimasaai Mchungaji Mark Murenga.
IMG_1383
Mama Mashuhuri kutoka kijiji cha Olopiri, Nolarir Pashuku, akitoa maoni yake kwenye kongamano.
IMG_1369
Mmoja wa washiriki katika warsha hiyo ambaye ni Laigwanan , John Olekulinja kutoka kata ya Malambo akizungumzia mafunzo hayo.
IMG_1357
Kiongozi wa Malaiboni wilaya ya Ngorongoro Bw. Sangau Naimodu (katikati) akieleza namna inavyofaa kueneza elimu ya mabadiliko.
IMG_1525
Mratibu wa Afya ya Uzazi na Mtoto, tarafa ya Loliondo (W) Ngorongoro, Bi. Nailejileji Joseph akitoa elimu ya uzazi wa mpango kwa washiriki wa kongamano hilo.
IMG_1351
Pichani juu na chini ni viongozi wa mila wa kabila la wamasai (Laigwanan/Ngaigwanan), Laiboni na wanawake Mashuhuri walioshiriki kwenye kongamano hilo yenye lengo la kushawishi uondoaji wa mila potofu zinazorudisha nyuma maendeleo katika jamii za wafugaji lilioandaliwa na Shirika la UNESCO.
IMG_1430
IMG_1471
IMG_1480
IMG_1294
 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa