Arusha
Home » » Uchaguzi mkuu, kura ya maoni kwa pamoja wapingwa vikali.

Uchaguzi mkuu, kura ya maoni kwa pamoja wapingwa vikali.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Mwenyekiti wa Nec, Jaji Mstaafu Damian Lubuva.
Kauli ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) kwamba kuna uwezekano wa kufanyika kwa pamoja kura ya maoni ya katiba inayopendekezwa na uchaguzi mkuu wa mwaka huu, limepingwa vikali na watu wa kada mbalimbali. 
 
Miongoni mwao wamo wasomi, wanasiasa na wanaharakati, ambao wengi wameonya kuwa, iwapo itatekelezwa kutawakanganya na kuwavuruga wananchi na hatimaye kuzua vurugu na machafuko nchini.
 
Walitoa maoni hayo katika mahojiano na NIPASHE yaliyofanyika kwa nyakati tofauti mikoa kadhaa nchini jana kufuatia kauli ya Mwenyekiti wa Nec, Jaji Mstaafu Damian Lubuva, katika mahojiano na gazeti moja la kila siku nchini 
 
Jumanne wiki hii.
MHADHIRI: ITAWAVURUGA WAPIGAKURA IRINGA
Mhadhiri Msaidizi wa Kitivo cha Sanaa na Sayansi ya Jamii ya Chuo Kikuu cha Iringa (UoI), Emanuel Damalo, alisema hoja hiyo ya Nec inaweza kuvuruga akili za wapigakura kwa kuwa itawalazimisha wafanye maamuzi yenye ukakasi.
 
“Huko ni kuwalazimisha Watanzania wapige kura ya maoni bila ya kutafakari na kufanya uamuzi sahihi. Kauli ya Lubuva (Mwenyekiti wa Nec) inaashiria kwamba, huo ndio uamuzi wa serikali na alichokifanya ni kudokeza ili kupima upepo wa kisiasa; kitu ambacho hakiwezekani kwa sasa,” alisema Damalo.
 
‘KUNA AJENDA YA SIRI’
Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Vijana wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo-Chadema (Bavicha), Patrick Ole Sosopi, alisema Nec inachopaswa kusisitiza kwa sasa ni juu ya uandikishaji wa Daftari la Kudumu la Wapigakura na siyo kuzungumzia kura ya maoni kwa kuwa inadhihirisha kuna ajenda ya siri nyuma ya kauli yake.
 
“Niseme kwamba, Nec wasijidanganye wataunganisha kura ya maoni ya katiba na uchaguzi mkuu na Watanzania wakakubali na kwenda kutekeleza jukumu hilo kwenye masanduku ya kura. La! hasha! Tutaipinga. Kwa sababu wanachotaka kukifanya ni kuusukuma umma ukibebe Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika chaguzi ili kisianguke madarakani,” alisema Ole Sosopi.
 
PROF. NKYA: HOJA  YA NEC NI DHAIFU
Mhadhiri Mstaafu wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Tiba na Sayansi ya Jamii cha KCMC, Prof. Watoki Nkya, alisema hoja ya Nec haiwezi kuushawishi umma kwa sasa kuafiki kuunganishwa kwa mambo hayo mawili, wakati katiba  ni tukio muhimu la kihistoria litakaloliongoza taifa kwa zaidi ya miaka 50 baadaye.
 
STOLLA: HAIWEZEKANI KUUNGANISHA MASUALA MAWILI 
Makamu wa Rais wa Chama cha Wanasheria Afrika Mashariki, Francis Stolla alisema haiwezekani kuyaunganisha masuala yote mawili kwa wakati mmoja, kwani yatawachanganya wananchi, ambao hawajawahi kukutana na jambo kama hilo tangu jadi yao.
 
Stolla ambaye aliwahi kuwa Rais wa Chama cha Wanasheria cha Tanganyika (TLS), alisema utekelezaji na usimamizi wa mambo yote mawili ni mgumu, kwani wakati wa uchaguzi kunakuwapo na mambo mengi, ukiwamo ucheleweshwaji wa vifaa vya kupigia kura katika baadhi ya vituo.
 
Hivyo, alipendekeza kumalizika kwanza kwa suala la uchaguzi mkuu na baada ya wananchi kupumzisha akili zao, ndipo kufuatiwe na suala la kura ya maoni kwa katiba inayopendekezwa.
 
WASOMI MBEYA WAPINGA
Mwenyekiti wa Mtandao wa Wasomi Mkoa wa Mbeya, Mzee Prince Mwaihojo, alisema hatua ya Nec kufikiria kuendesha kura ya maoni sambamba na uchaguzi mkuu haifai, kwani inaweza kusababisha madhara makubwa kwa jamii.
 
“Tukifikiri mambo kwa kina tunaona kwamba, Nec inataka kuwaondoa wananchi kwenye uchaguzi mkuu ili wajikite kwenye katiba. Hali hiyo haifai kabisa kwa sababu wananchi watajikuta wakifanya mambo yote mawili, huku fikra zao zikiwaza jambo moja. Matokeo yake suala mojawapo halitafanyika kwa ufanisi,” alisema Mzee Mwaihojo.
 
WAKILI SHITAMBALA: ITALETA MFARAKANO
Wakili wa Kujitegemea na mwanasiasa mzoefu mkoani Mbeya, Sambwee Shitambala alisema yeye siyo shabiki wa kuona kura ya maoni inafanyika siku moja na uchaguzi mkuu kwa sababu ana amini huo utakuwa ni mchakato wenye mfarakano.
Alisema Nec imekuwa haiaminiki, kuanzia matamshi yake mpaka matendo yake, jambo ambalo linawawia vigumu Watanzania kuiamini.
 
Shitambala ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mbeya, alipendekeza kuwa kabla ya kufikiria ni lini kura ya maoni itapigwa, kwanza Nec ielekeze nguvu zake katika kukamilisha uandikishaji wa wapigakura.
 
MWANAFUNZI TEKU: NI VIGUMU
Mwanafunzi wa sheria mwaka wa pili katika Chuo Kikuu cha Teofilo Kisanji (Teku) cha jijini Mbeya, Samwel Jonathan, alisema ni vigumu kwa Nec kuendesha kura ya maoni siku moja na uchaguzi mkuu kutokana na tume yenyewe kutokuwa na umakini, rasilimali za kutosha na kuingiliwa na viongozi wa serikali kila wakati.
 
Alisema ikiwa uchaguzi mkuu wenyewe huitoa jasho Nec kiasi cha kuonyesha upungufu mkubwa katika baadhi ya maeneo, siyo rahisi kwa tume hiyo hiyo kufanya kazi zote mbili kwa wakati mmoja na ikafanikiwa.
 
LOISULIE: ITALETA MKANGANYIKO
Mwenyekiti wa Jumuiya za Wanataaluma Tanzania (ASAs) Paul Loisulie, alisema ni matukio mawili yenye uzito mkubwa kwa taifa, hivyo havihitaji kuchanganywa.
 
 “Jaribio lolote la kuchanganya hivi viwili ni kudharau uzito wa masuala haya. Na athari ni pamoja na kukosesha wananchi fursa ya kufuatilia kila tukio na kujenga uelewa, hasa katiba inayopendekezwa,” alisema Loisulie.
 
 CHACHA: KURA YA MAONI ISOGEZWE MBELE
Mwenyekiti wa Umoja wa Wanataaluma katika Chuo Kikuu cha Dodoma (Udomasa), Nashon Chacha, alishauri Nec kutokaribisha wazo la kuahirisha uchaguzi au kuchanganya kura ya maoni ya katiba mpya na uchaguzi kwa madai muda hautoshi. 
 
KABUTARI: NI KULIPASUA TAIFA
Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Ukombozi wa Umma (Chaumma), Kayumbo Kabutari, alisema lengo la kura ya maoni lililokuwa kupata katiba mpya itakayotumika kwenye uchaguzi mkuu 2015 limeshindikana, hivyo hakuna haja ya kulipasua taifa.
 
NYAMBABE: NI MKAKATI  KUIBA KURA 
Katibu Mkuu wa Chama cha NCCR-Mageuzi, Mosena Nyambabe, alisema huo ni mkakati, ambao umepangwa kwa ajili ya kuwaibia Watanzania kura.
 
Alisema wanataka kufanya hivyo ili kuwapumbaza Watanzania waegemee zaidi  katika kitu kimoja ili  wao wapate mwanya wa kuiba kura.
 
Nyambabe alisema hata wakifanya hivyo watakuwa wamekiuka sheria ya kura ya maoni, ambayo inabainisha kwamba, kabla ya kufanyika kura hiyo, ni lazima wananchi waandikishwe kwenye daftari ambalo mpaka sasa halipo na kutolewa kwa elimu ya uraia na mwezi mmoja wa kampeni.
 
MWAKAGENDA: ITASABABISHA VURUGU
Jukwaa la Katiba Tanzania (Jukata) limesema kufanyika kwa kura ya maoni pamoja na uchaguzi mkuu Oktoba, mwaka huu ni uvunjifu wa sheria na kunaweza kusababisha vurugu kubwa wakati wa michakato hiyo.
 
Kaimu Mwenyekiti wa Jukata, Hebron Mwakagenda, alisema kura ya maoni na uchaguzi mkuu vina sheria mbili tofauti, hivyo hatua hiyo itawachanganya wananchi.
 
WASOMI: ITAZUA VURUGU
Mmoja wa wasomi kutoka Chuo Kikuu Huria (OUT), Aziz Habibu, alisema uamuzi wa kuunganisha vitu viwili kwa pamoja unaweza kutoa nafasi ya kuwapo kwa vurugu kwa kuwa unashirikisha vitu viwili kwa wakati mmoja.
 
Alisema tayari mchakato wa kura ya maoni ulishaingia dosari katika eneo lililofanyiwa majaribio, hivyo kuunganishwa na uchaguzi mkuu kunaweza kusababisha kuwapo kwa uvunjifu wa amani.
 
Barnabas Kasera kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (Sua) alisema amestushwa na maamuzi ya Nec kwa kuwa tayari mchakato wa kura ya maoni umeshashindikana kutokana na mfumo unaotumiwa kusuasua kutokana na uchache wa mashine.
 
Joel Mlambiti kutoka Chuo Kikuu cha Mzumbe alisema ameshangazwa na Nec kuendelea kung’ang’ania kura ya maoni wakati tayari mchakato wa majaribio ulishashindikana kutokana na ufinyu wa vifaa.
 
Alisema uchaguzi mkuu mara zote huwa na mambo mengi, ikiwamo yanayohusu vyama vya siasa kufanya kampeni na kwamba wakati mwingine kumekuwapo na maeneo ambayo yamekuwa na uvunjifu wa amani.
 
MGAYA: NI KUWAKOROGA WANANCHI
Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (Tucta), Nicholaus Mgaya, alisema kufanyika kwa pamoja kura ya maoni ya katiba inayopendekezwa na uchaguzi mkuu ni kuwachanganya wananchi kwa sababu kila jambo lina ukubwa wake na umuhimu wake.
 
“Siyo sawa kuwapigisha kura mbili Watanzania; ya katiba na uchaguzi mkuu, hasa ikizingatiwa kuwa mambo yote haya ni muhimu kwa taifa letu. Ni vyema likafanyika jambo moja kwanza la uchaguzi ndipo lifuate la katiba ili Watanzania wapate muda wa kuisoma na kuichambua,” alisema Mgaya. 
 
POLEPOLE: NI VITU TOFAUTI 
Aliyekuwa mjumbe wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Humphrey Polepole, alisema kura ya maoni ya katiba inayopendekezwa na ile ya uchaguzi mkuu ni vitu viwili, ambavyo haviwezi kuchanganywa.
 
Alisema mchakato wa kupiga kura katika uchaguzi mkuu ni tendo la kisiasa, ambalo litakwenda kuwapata wabunge, madiwani na rais, lakini kitendo cha kupiga kura ya maoni ya katiba inayopendekezwa ni cha kisiasa, lakini halihusishi vyama vya siasa.
 
Alisema vyama vya siasa pindi vinapofarakana hukimbilia kupata muafaka, hivyo mchakato wa katiba inayopendekezwa ukijumuishwa katika mchakato wa uchaguzi mkuu, utawapa mwanya wanasiasa kuingiza mambo yao yatakayowasaidia.
 
“Ni mwiko kuingiza siasa katika katiba. Tukifanya hivyo tutageuza mchakato kuwa agenda ya kisiasa,” alisema Polepole.
 
Aliishauri Nec kuwa mwaka huu ni ngumu kupata katiba mpya kabla ya uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba.
Hivyo, alilishauri Bunge kuifanyia marekebisho katiba ya mwaka 1977 ili itumike katika uchaguzi mkuu wa Rais, wabunge na madiwani.
 
HELLEN KIJO-BISIMBA: HAIWEZEKANI 
Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk. Hellen Kijo-Bisimba alisema kufanya kwa pamoja upigaji kura ya maoni ya katiba inayopendekezwa na uchaguzi mkuu haiwezekani kwa kuwa kila jambo linatakiwa kupewa nafasi yake kutokana na umuhimu wake kwa taifa.
 
Alisema michakato yote miwili ikifanyika kwa pamoja itachanganya wananchi, hasa kutokana na ugeni wa kura ya maoni ya katiba na kusisitiza bado elimu haijatolewa kwa makundi husika kuyawezesha kufanya uamuzi sahihi.
 
“Katiba inayaopendekezwa na uchaguzi mkuu ni vitu viwili tofauti vikichanganywa, vitaleta mkanganyiko kwa wananchi sababu ya uelewa mdogo walionao. Ni bora kila jambo likapewa nafasi yake,” alisema Dk. Bisimba.
 
Alishauri kuwa ni bora mchakato wa kura ya maoni ya katiba inayopendekezwa ukaahirishwa mpaka mwishoni mwa mwakani wakati nchi itakuwa imepata viongozi wapya watakaofanya mipango ya kutoa elimu ipasavyo na kulisaidia taifa kupata katiba inayotokana na maoni ya wananchi.
 
DK. BANA: VITENGANISHWE KWA MUDA
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Kitengo cha Sayansi ya Jamii, Dk. Benson Bana, alisema kura ya maoni kwa katiba inayopendekezwa na uchaguzi mkuu haviwezi kwenda pamoja, ila vinaweza kutenganishwa kwa muda mfupi.
 
Alisema kwa kuiga mfano wa Zanzibar, ambao mwaka 2010 walifanya kura ya maoni Julai na uchaguzi mkuu Oktoba, hivyo kura ya maoni inaweza kufanyika Agosti na uchaguzi mkuu Oktoba, mwaka huu.
 
Dk. Bana alisema ni suala la makubaliano ili kumfanya Rais Kikwete, ambaye ndiye aliyeanzisha mchakato huo kuondoka madarakani akiwa amemaliza kuliko kubebesha zigo hilo kwa kiongozi mwingine ajaye.
 
Imeandkwa na Godfrey Mushi, Moshi; Emmanuel Lengwa, Mbeya; Ashton Balaigwa, Morogoro; Augusta Njoji, Dodoma; Isaya Kisimbilu, Elizabeth Zaya, Christina Mwakangale, Mary Geofrey, Enles Mbegalo, Gwamaka Alipipi, Salome Kitomari na Hussein Ndubikile, Dar.
 
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa