Arusha
Home » » SERA YA ELIMU NA TUME YA AJIRA KWA WALIMU MBIONI KUKAMILIKA

SERA YA ELIMU NA TUME YA AJIRA KWA WALIMU MBIONI KUKAMILIKA

 
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Jamii, Margareth Sitta.
Serikali imesema iko katika hatua za mwisho za kukamilisha sera mpya ya elimu na uundwaji wa Tume ya Ajira kwa Walimu (TSC) inayotarajiwa kuanza Julai, mwaka huu.
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Jamii, Margareth Sitta, alitoa kauli hiyo kwa waandishi wa habari, baada ya kamati yake kumaliza kukutana na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Utumishi na Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB).

Alisema kamati yake umepokea taarifa ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, ikiongozwa na Naibu Waziri, Jenista Mhagama, na wataalamu ambao walieleza kuwa wako katika hatua za mwisho za kukamilisha sera ya elimu.

Alisema Waziri Celine Kombani aliieleza kamati hiyo kuwa uundwaji wa Tume ya Ajira kwa walimu umefikia hatua ya mwisho na Julai mwaka huu itazunduliwa.

Sitta alisema chombo hicho ni kilio kikubwa kwa walimu kwa kuwa kumekuwa na vyombo vingi vya kuwahudumia na hivyo kusababisha usumbufu mkubwa.

“Katika kikao cha Bunge la Bajeti cha Mei, mwaka jana, kamati yangu ilishikilia Bajeti ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi ikitaka kauli ya serikali kuwa ni lini itaunda chombo cha kuhudumia walimu, serikali imetuhakikishia kuwa kila kitu kimekamilika na sasa litaanza hivi karibuni, hii ni habari njema kwa walimu," alisema.

"Hakuna uwezekano wowote wa kutekeleza Mpango wa matokeo makubwa sasa (BRN), bila kuwahudumia walimu inavyotakiwa, matatizo ya walimu ni mengi na yana kosa chombo kimoja cha kuhudumia," alisema mwenyekiti huyo.

Katika kikao cha Bunge Mei 20, mwaka huu, Sitta alitoa Shilingi na kueleza kuwa kukosekana chombo Maalum cha kuhudumia walimu kumesababisha walimu kudhulumiwa haki zao za msingi na kwa miaka mitatu kamati yake imeomba ila inapigwa danadana.

Sitta alisema pia wamekutana na HESLB ambayo imeomba muda wa kufanyia kazi suala la utoaji mikopo kwa walimu wa Sayansi na Hisabati ngazi ya stashahada kwamba kwa sasa maofisa mbalimbali wanatembelea vyuo kufanya uchunguzi ndipo watoe taarifa kwenye kamati mwishoni mwa mwezi huu.

CHANZO: NIPASHE
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa