Arusha
Home » » BAADA YA MIAKA 20, MARIDHIANO YASAKWA LOLIONDO

BAADA YA MIAKA 20, MARIDHIANO YASAKWA LOLIONDO

 
 Kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012, Wilaya ya Ngorongoro ilikuwa na jumla ya wakazi 174,278 ikiwa na eneo la kilomita za mraba 14,036. Asilimia 52 ya ardhi yake ni hifadhi ya wanyamapori.

Wilaya hii yenye tarafa tatu za Loliondo, Ngorongoro na Sale, wakazi wake wanatumia asilimia 48 ya ardhi iliyobaki kwa shughuli za ufugaji. Ni sehemu ndogo ya ardhi hasa Sale ambayo wakazi wake wanatumia ardhi kwa shughuli za kilimo.
Kwa sababu ya kuongezeka kwa watu na mifugo, mahitaji ya eneo la malisho na kilimo nayo yanakua siku hadi siku.
Leo tutazungumzia mgogoro mmoja baina ya kata saba na kampuni ya ya Ortello Business Cooperation (OBC,) licha ya eneo hilo kuwa na kampuni zaidi ya tano zenye maslahi tofauti.
Kampuni hii ya OBC ndiyo imekuwa ikiendesha uwindaji wa kitalii katika eneo la pori Tengefu Loliondo. Mwaka huu, mgogoro ulikuwa mkubwa zaidi hasa baada ya Serikali kupitia aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki kulipunguza eneo la pori tengefu la Loliondo kutoka kilomita za mraba 4,000 hadi 1,500 .
Katika uamuzi huo, Serikali ilisema eneo la kilomita za mraba 2,500 litabaki kwa wakazi wa Loliondo na Sale na eneo la kilomita za mraba 1,500 litabaki chini ya Serikali kwa ajili ya uhifadhi ili kulinda mazalia na mapito ya wanyamapori.
Eneo hilo la kilomita za mraba 1,500 zinapakana na Hifadhi ya Taifa ya Serengeti upande wa Mashariki na pia linapakana na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro.
Eneo hilo linachangia kwa kiwango kikubwa kuimarisha mfumo wa ikolojia wa Serengeti ambao unaruhusu wanyama kuhama kutoka ndani ya hifadhi na kuingia katika eneo hili kwa malisho na mazalia hasa nyakati za masika.
Tangazo hilo la Serikali, liliibua malalamiko ya wananchi wa Loliondo wakiungwa mkono na mashirika kadhaa yasiyo ya kiserikali ya ndani na nje ya wilaya. Wapingaji wa tangazo hilo, walisema Serikali imekiuka Sheria ya Ardhi ya mwaka 2009 na pia Sheria ya Wanyamapori ya mwaka 2009.
Malalamiko hayo yalisababisha Serikali kuingilia kati baada ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kwenda Loliondo Aprili mwaka jana na kutengua uamuzi wa awali kuligawa eneo hilo.
Pia, Chama cha Mapinduzi (CCM), mapema mwaka jana, kiliunda tume ya kuchunguza mgogoro huo. Tume hiyyo iliongozwa na Naibu Katibu Mkuu, Mwigulu Nchemba.
Tume hiyo ilipokutana na wananchi na viongozi wa eneo hilo, ilikumbana na tishio kubwa la wanachama wa CCM kukihama chama hicho baada ya kukabidhiwa rundo la kadi za chama.
Maridhiano
Baada ya kuendelea mgogoro kwa huu bila ya mwafaka, Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyarandu alizindua vikao vya maridhiano.
Akitumia kauli mbiu yake, ‘Ngorongoro bila migogoro inawezekana’, anatangaza kuunga mkono, uamuzi wa kata tatu, za Oloipili, Losoito Maalon na Olorieri Magaidulu kuamua kuanza kushirikiana na wawekezaji wa wilaya hiyo, kwa manufaa ya wananchi.
Nyalandu anasema haiwezekani miaka zaidi ya 20 Loliondo, iendelee kusifika kwa migogoro ambayo imekuwa ikisababishwa na watu wachache kwa masilahi yao.
“Ni lazima sasa mkubali kukaa viongozi wa kata zote saba ambazo zinapakana na mwekezaji OBC na wengine na kujadiliana mambo ya msingi kwa masilahi ya pande zote,” anasema.
Anasema ni muhimu mwekezaji akazingatia taratibu na sheria katika eneo lake kwani Serikali haitamvumilia mwekezaji ambaye hana uhusiano mwema na jamii, lakini pia ni lazima wananchi wajue kwamba wanapaswa kufuata sheria na taratibu katika makazi yao.
Nyalandu, anatoa wito kwa wakazi wa tarafa hiyo, kuendelea kuishi bila hofu, kwani Serikali haina mpango wa kuwaondoa kama ilivyotangazwa na vyombo vya habari vya kimataifa na kutoa ardhi yao kwa mwekezaji yoyote.
“Hakuna mpango wa kuwaondoa leo wala kesho na kutoa ardhi hii kwa mwekezaji kutoka Falme za Kiarabu, tunawataka muishi bila hofu na hakuna ambaye anaondolewa na kuchomewa makazi hapa Loliondo, kikubwa tunataka migogoro imalizike,” anasema .
Madiwani waliotangaza kujitenga na mgogoro
Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Ngorongoro, Raphael Long’oi anasema wamechoshwa na migogoro isiyokwisha ambayo inachangiwa na watu wachache kwa masilahi yao.
Long’oi ambaye ni Diwani wa Losoito Maalon, anasema kata yake na zile za Oloipili na Olorieni wamekubaliana kuachana na migogoro na wawekezaji kwa manufaa ya wananchi.
Hata hivyo, anaiomba Serikali iliwalinde kutokana na vitisho kutoka kwa kundi ambalo halitaki maridhiano ambalo sasa linabadilisha maridhiano yao na kutangaza wao kama viongozi wanauza ardhi kwa wawekezaji.
Diwani wa Kata ya Oloipili, William Alais anasema kwake hakuna mgogoro na wawekezaji na taarifa nyingi ni za uchochezi zinazowanufaisha watu wachache.
Alais anasema wamefikia maridhiano na wawekezaji na wameanza kunufaika na miradi ya maendeleo.
“Wanaochechea ni watu wachache, kwa manufaa yao sasa sisi tumekubaliana kusema hatutaki migogoro tunataka maendeleo”anasema
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Ngorongoro, Elias Ngolisa anasema wanachohitaji wananchi wa Ngorongoro ni kuishi maisha yao kama zamani bila kuhamishwa.
“Kama wananchi hawa wakiachwa katika ardhi yao, sidhani kama kutakuwa na mgogoro Loliondo, sisi tunataka maendeleo,” anasema.
Ngolisa ambaye ni Diwani wa Malambo, kata ambayo haijafikia maridhiano na mwekezaji OBC, anasema atashiriki kikao cha maridhiano ambacho kinashirikisha pia viongozi wa kata nyingine ambazo bado hazijafikia maridhiano za Arash, Soitsambu na Ololosokwani.
Mtandao wa mashirika watoa msimamo
Kwa miaka kadhaa, Serikali imekuwa ikiyatupia lawama mashirika yasiyo ya kiserikali Ngorongoro na kuyataja yamekuwa chanzo cha vurugu kutokana na kutoa taarifa za uchochezi, ikiwamo upotoshwaji juu ya taarifa kuwa wananchi 40,000 wa Loliondo wanatakiwa kuondolewa kumpisha mwekezaji.
Mratibu wa mashirika yasiyo ya kiserikali Wilaya ya Ngorongoro (Ngonet), Samweli Nang’irwa anakanusha madai hayo.
Anasema mashirika yao yakiwa wadau wa maendeleo, hayapingani na mwekezaji yoyote, bali wanataka wawekezaji wafanye majukumu yao na wananchi waendelee na maisha yao.
Nang’irwa ambaye hivi karibuni, alikamatwa na kuhojiwa kwa saa zaidi ya tatu kuhusiana na mgogoro huo, anasema mashirika yao, yanajihusisha na masuala ya maendeleo ya jamii na utetezi, hivyo kama wananchi wakifikia maridhiano na wawekezaji wao hawana matatizo.
OBC wataka maridhiano

Kampuni ya OBC inaungana na Serikali na madiwani wa kata tatu kutaka maridhiano ili kila upande uendelee na shughuli zake kwa manufaa ya pande zote .
Mkurugenzi Mtendaji wa OBC, Isack Mollel anasema tangu kampuni hiyo iliposaini mkataba huo, imekuwa ikiwinda kitalii chini ya usimamizi wa Serikali kama zilivyo kampuni nyingine.
Mollel anasema, eneo la pori tengefu lina historia ndefu kwani awali, lilikuwa chini ya shirika la umma la uwindaji wa kitalii la Tawico ambalo sasa tayari limebinafsishwa.
“OBC tangu tumefika Loliondo licha ya uwindaji, tumefanya mengi. Hakuna kampuni ya uwindaji nchini ambayo imefanya vitu vingi kama sisi. Tumejenga sekondari, tumetoa misaada mingi katika sekta ya afya, maji na elimu na uhifadhi,’’ anaeleza.
 Chanzo:Mwananchi
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa