Arusha
Home » » PFF YAZIBEBA FAMILIA ZA WALIOTANGULIA MBELE ZA HAKI

PFF YAZIBEBA FAMILIA ZA WALIOTANGULIA MBELE ZA HAKI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
MFUKO wa Pensheni wa PPF, umetumia zaidi ya sh milioni 770 kugharamia masomo ya watoto 1,100 wa wanachama wa mfuko huo waliyofariki wakiwa kazini.
Aidha, mapato ya uwekezaji ya mfuko huo yameongezeka kwa asilimia 174.5 kutoka sh bilioni 111.1 zilizopatikana mwaka 2012 hadi kufikia sh bilioni 305.2 mwaka 2013.
Hayo yalisemwa juzi na Mwenyekiti wa bodi ya wadhamini wa mfuko huo, Ramadhani Khijjah, wakati akizungumza kwenye mkutano wa 24 wa mwaka wa wanachama na wadau wa mfuko huo unaofanyika jijini hapa kwa siku tatu.
Alisema kuwa watoto hao wamegharamiwa masomo kuanzia shule za awali mpaka kidato cha sita kwenye shule mbalimbali hapa nchini.
Khijjah, alisema kuwa katika kipindi cha kuanzia Januari hadi Juni mwaka huu, mapato yatokanayo na uwekezaji yamefikia sh bilioni 136.62 ambako lengo ni kukusanya sh bilioni 172.36 kwa mwaka 2014.
Alisema kuwa, mfuko huo hutumia zaidi ya sh bilioni 4.1 kila mwezi kwa ajili ya kulipa wastaafu wake 24,981 hivyo kuwawezesha kumudu kukidhi kiwango cha mahitaji yao muhimu ya maisha.
Mwenyekiti huyo wa bodi, alisema kuwa mfumo wa  PPF umewekeza kwa kununua hisa kwenye taasisi za fedha ikiwemo benki ya CRDB, Azania na Benki ya Akiba, ambako hadi Juni mfuko huo kwenye taasisi hizo zimefikia thamani ya sh bilioni 80.263 huku ukiwa na amana za sh bilioni 281.57 katika mabenki 30 hapa nchini.
Katika siku ya kwanza ya mkutano huo,  Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Mchemba, alizindua huduma za PPF za miito ya simu na matumizi ya PPF itakayowawezesha wanachama kupatiwa taarifa kupitia simu za mkononi na ipad, (PPF taarifa mobile App)
Chanzo:Tanzania Daima 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa