Arusha
Home » » MBOWE ATUMIA MIL.250/- SHUGHULI ZA MAENDELEO

MBOWE ATUMIA MIL.250/- SHUGHULI ZA MAENDELEO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399
Mbowe atumia mil. 250/- shughuli za maendeleo MBUNGE wa Hai, Freeman Mbowe (CHADEMA), ametumia sh milioni 256.7 jimboni humo kwa ajili ya kuchangia shughuli za maendeleo ambapo sekta ya elimu imeongoza kwa kupata asilimia 37.76 ya fedha zote.
Hayo yalisemwa mwishoni mwa wiki na Katibu wa mbunge huyo, Ndonde Totinan kwenye mkutano mkuu wa wilaya wa CHADEMA wakati alipotoa taarifa ya utendaji wa ofisi ya mbunge kwa mwaka 2010 hadi Juni 30, mwaka huu.
Alisema ofisi hiyo ilizipatia fedha sekta nyingine za barabara, miti na mazingira, afya, maji, vijana na kusaidia makanisa na misikiti.
“Katika fedha hizo sh milioni 125.8 zinatoka kwenye mfuko binafsi wa Mbowe ambaye pia ni Kiongozi wa Upinzani Bungeni (KUB) na sh milioni 130.9 zinatokana kwenye mfuko wa jimbo unaosimamiwa na mbunge huyo,” alisema.
Totinan alisema katika kipindi cha mwaka mmoja uliobaki kabla ya uchaguzi mwakani, Mbowe anatarajia kuwawezesha wananchi kuanzisha miradi ya kuku, vikundi vya kuweka na kukopa (Saccos) ya vijana na kuboresha shughuli za usafi wa mazingira.
Alisema sekta ya elimu ilitengewa sh milioni 96.9 ambapo kata zote 14 za Hai zilinufaika kulingana na ahadi alizotoa mbunge wakati wa kampeni.
Alisema fedha hizo zilitumika kusaidia ujenzi wa madarasa, nyumba za walimu, jiko, vyoo, kununua mashine ya kurudufisha (photocopy machine) na ununuzi wa samani za ofisi kwenye baadhi ya kata.
Kwa mujibu wa katibu huyo, Mbowe alinunua trekta la sh milioni 70 kwa ajili ya kusimamia programu ya miti na mazingira na shughuli nyingine za kijamii ukiwemo ujenzi wa barabara na shule za jimbo hilo ambapo linatumika pia kubeba taka kwenye soko la Kwa Sadala na Hai Mjini.
Upande wa barabara, Mbowe alitumia sh milioni 60.1 kwa ajili ya ujenzi wa vivuko na madaraja kuhakikisha zinapitika kipindi chote cha mwaka
Chanzo:Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa