Arusha
Home » » DCI:MABOMU ARUSHA SIYO AL-SHABAAB

DCI:MABOMU ARUSHA SIYO AL-SHABAAB

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) wa Jeshi la Polisi nchini, Isaya Mngulu.
 
Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) wa Jeshi la Polisi nchini, Isaya Mngulu, amesema matukio ya ulipuaji wa mabomu yanayotokea katika Jiji la Arusha hayana uhusiano na matukio ya kigaidi yanayotokea nchi jirani ya Kenya.
Alisema hayo jana wakati akihojiwa katika kipindi cha Kumepambazuka kinachorushwa na Radio One Stereo kila siku asubuhi.

Nchini Kenya kumakuwapo na matukio ya mara kwa mara ya kigaidi yanayodaiwa kufanywa na kikundi cha Al Shabaab na watu kadhaa wameshapoteza maisha kutokana na matukio hayo.

 Mngulu alisema matukio ya ulipuaji wa mabomu siyo ya ugaidi kama inavyoelezwa na baadhi ya watu na wala hayafanywi na watu kutoka nje ya nchi, bali ni watu waliopo hapa nchini, ambao wanataka kuona amani ya nchi inavurugika.

“Matukio ya mabomu Arusha hayana uhusiano na matukio kikagidi kama yanayotokea nchini Kenya. Pia hayana uhusiano na masuala ya kisiasa,” alisema Mngulu.

Alisema uchunguzi uliofanywa na  Polisi umebaini kuwapo kwa kikundi kinachojihusisha na matukio hayo na kwamba, jeshi hilo litahakikisha watuhumiwa wote wanasakwa na kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.

Aliwaomba wananchi kutoa ushirikiano kwa jeshi hilo ili kufanikisha kuwakamata watuhumiwa wa matukio hayo, kwani suala la ulinzi na usalama ni jukumu la kila mwananachi.

Usiku wa kuamkia jumatatu wiki hii, kulitokea mlipuko mwingine wa bomu uliojeruhi watu wanane jijini Arusha.Kati ya hao mmoja amelazimika kukatwa mguu katika Hospitali ya Rufaa ya Selian na hali yake ni mbaya.
Tukio lilitokea siku tano tangu bomu lingine liliporushwa Julai 3, mwaka huu, saa 5 usiku na kuwajeruhi watu wawili; Sheikh Sudi Ally Sudi (37) nyumbani kwake, mtaa wa Majengo Chini wakati akipata daku pamoja na rafiki yake, Muhaji Hussein Kifea (38), ambaye ni mkazi wa Sinza, jijini Dar es Salaam aliyekuwa akitokea Nairobi, Kenya.

Sheikh huyo wa Msikiti wa Qiblatan, uliopo eneo la Kilombero, jijini Arusha na rafiki yake, walijeruhiwa vibaya maeneo ya miguuni na kulazwa Hospitali ya Mkoa wa Arusha ya Mount Meru, lakini sasa wamehamishiwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) kwa matibabu zaidi.

Akizungumzia tukio hilo la jumatatu majeruhi hao walilipukiwa na bomu hilo wakiwa katika mgahawa wa Kituo cha Vama Indian Traditional, kilichopo majengo ya Gymkhana, kinachotazamana na Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Mtaa wa Uzunguni, ambako kuna Ikulu ndogo na nyumba ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha.

WATUHUMIWA 16 WA MABOMU WANYIMWA DHAMANA
Katika hatua nyingine; watuhumiwa wanaodaiwa kuhusika na matukio ya ulipuaji wa mabomu, kwa mara nyingine jana walipandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha na kunyimwa dhamana.

Mbele ya Hakimu wa Mahakama hiyo, Devote Msofe watuhumiwa walinyoosha kidole na alipowaruhusu kuongea, waliomba kufahamu hatma ya dhamana yao.

“Mheshimiwa hakimu, tunataka kujua. Lini tutapata dhamana? Au kesi hii haina dhamana? Pia baadhi yetu hatuna nakala ya hati ya mashitaka. Tunaomba tupatiwe, maana ni haki yetu ya msingi,” mmoja wa watuhumiwa hao alidai kwa niaba ya wenzao.

Akijibu hoja hiyo, Hakimu Devota alisema kesi yao haina dhamana.Kuhusu hati ya mashitaka, Hakimu Devote alisema mahakama itawapatia wote.“Kweli kabisa kesi yenu haina dhamana. Na kama mna hoja nyingine,Niambieni. Ila kuhusu nakala ya hati ya mashitaka, nitawapatieni leo hii hii, maana ni haki yenu ya msingi,” alisema Hakimu devote.

Awali Mwendesha mashitaka wa Serikali, Gaudencia Joseph alidai mahakamani hapo kuwa kuwa watuhumiwa Abdulkarimu Hasia na Abdallah Wambura hawakuweza kufika mahakamani kutokana na kuendelea kuugua maradhi ambayo hakuyataja.

Aliwataja watuhumiwa wengine katika kesi hiyo kuwa nmi  Abdallah Athumani, Swalehe Hamisi, Abdallah Yasini, Hassani Saidi, Sudi Lusuma, Abdulkarim Hasia na Shaban Wawa.

Wengine ni Hassan Zuberi Saidi, Rajab Phiri Hemedi, Ally Hamisi Kidaanya, Abdallah Maginga Wambura, Shabani Abdallah Wawa, Ally Hamisi Jumanne na Yassin Hashim Sanga.

Kesi hiyo imeahirishwa kutokana na uchunguzi kutokamilika hadi julai 24, mwaka huu, itakapotajwa tena.Kwa mujibu wa hati ya mashtaka, watuhumiwa wanadaiwa kulipua mabomu kati ya mwaka 2010 hadi Februari, mwaka huu, maeneo mbalimbali nchini, kinyume cha kifungu cha 118 (1) (a) cha Sheria ya Kuzuia Ugaidi ya mwaka 2002.

Pia wanadaiwa walijaribu kusajili watu kujiunga na kikundi cha kigaidi kinyume cha kifungu namba 21 (a) cha Sheria ya Kuzuia Ugaidi ya mwaka 2002.

Watuhumiwa hao pia wanadaiwa walimuua Sudi Ramadhan, ambaye alifariki dunia akiwa anapata matibabu Hospitali ya Mkoa wa Arusha ya Mount Meru Mei 13, mwaka huu.

Aidha, ilidaiwa mahakamani hapo kuwa watuhumiwa hao, walijaribu kuwaua watu 14 katika tukio la mlipuko wa bomu, kinyume cha kifungu cha 211 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

Tukio la mlipuko wa bomu, ulitokea Aprili 13, mwaka huu, katika baa Arusha Night Park iliyopo Mianzini, majira ya 1:30 usiku.
SOURCE: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa