Arusha
Home » » ATC CHAONGEZA KIWANGO UDAHILI WANAFUNZI WA KIKE

ATC CHAONGEZA KIWANGO UDAHILI WANAFUNZI WA KIKE

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Chuo cha Ufundi Arusha (ATC), kimeongeza udahili wa wanafunzi wa kike kufikia kiwango cha asilimia 30 katika mwaka wa masomo 2014/15.
Mkuu wa chuo hicho, Mhandisi Dk. Richard Masika, alisema mipango iliyowawezesha kufikia idadi hiyo ni pamoja na kuwawezesha wasichana/wanawake waliofaulu masomo ya Sayansi ya kidato cha nne lakini ufaulu wao siyo kwa kiwango cha kukidhi vigezo vya udahili wa moja kwa moja.

Alikuwa akizungumza kwenye hafla fupi ya kufunga mafunzo unganishi na kozi ya awali kwa ajili ya kujiunga na mafunzo ya stashahada ya uhandisi kwa mwaka wa masomo 2014/15.

Alisema chuo kimewapa wasichana hao mafunzo ya awali ya wiki nane katika masomo ya Sanyansi, na baadaye kufanya mitihani na kupata udahili wa kujiunga na masomo hayo pale wanapofaulu.

Pia alisema chuo kilihamasisha na kutangaza udahili wa wanafunzi wa kike kupitia kozi ya awali ambapo jumla ya maombi 131 yalipokelewa na kati yao 93 walikidhi vigezo vilivyowekwa na waliodahiliwa katika kozi hiyo ya awali ni 78.

Hata hivyo, alisema kwa bahati mbaya wanafunzi wote wa kike waliofaulu kozi ya awali na kudahiliwa hawatapata malazi kutokana na nafasi finyu za malazi kwani bweni la wanafunzi wa kike lina nafasi 186 tu za kulala ambazo tayari zimejaa.

Katika risala yao, wanafunzi hao waliiomba serikali na uongozi wa chuo hicho kuhakikisha kinajenga mabweni ya kutosha kwa ajili ya wanafunzi au wafanye mazungumzo na mashirika ili yajenge hosteli kwa kuwa mazingira yanayokizunguka chuo hicho si rafiki kwa masomo.

Walisema eneo linalozunguka chuo hakuna hosteli ambayo ingeweza kuwasaidia kupata sehemu ya malazi na kwenda kusoma kwa urahisi lakini badala yake eneo hilo limezungukwa na biashara za baa, nyumba za kulala wageni na maduka.

Mwenyekiti wa Bodi ya ATC, Abraham Nyanda, alisema, itaendelea kuyashawishi mashirika yanayojenga nyumba kama vitega uchumi, yaanze sasa kuwekeza katika ujenzi wa hosteli zitakazowawezesha wanafunzi wa kike na kiume kupata malazi ili waweze kuendelea na masomo yao.

Alisema bodi yake ilianza mazungumzo na mashirika kadhaa kuhusu suala hilo, na akaahidi kuendelea kujenga hoja zaidi ili kuyaelewesha mashirika hayo yaweze kutambua umuhimu wa kuwekeza katika ujenzi wa hosteli za wanafunzi.
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa