Arusha
Home » » 25 MBARONI KWA ULIPUAJI MABOMU

25 MBARONI KWA ULIPUAJI MABOMU

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 

JESHI la Polisi mkoani Arusha, linawashikilia watu 25 wanaodaiwa kujihusisha na matukio ya ulipuaji mabomu katika maeneo mbalimbali akiwemo mume na mke ambao walikutwa na mabomu saba pamoja na vifaa vyake kutoka nchi za Ujerumani na Urusi.

Mbali ya wanandoa hao kukutwa na mabomu hayo, pia Imamu wa Msikiti wa Quba, naye anashikiliwa na jeshi hilo kwa makosa ya kujihusisha na mtandao wa ulipuaji wa mabomu jijini Arusha.

Kukamatwa kwa watu hao na mabomu yaliyokuwa tayari kulipuliwa, kumetokana na msako unaoendelea kufanywa na jeshi hilo baada ya kupewa taarifa kutoka kwa raia wema.

Akizungumza na waandishi wahabari jana, Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), Isaya Mngulu, alisema watu hao walikamatwa kwa nyakati tofauti ila mabomu hayo yamepatikana eneo la Sombetini.

Alisema kupatikana kwa mabomu hayo, kunatokana na taarifa kutoka kwa raia wema ambapo Julai 21 mwaka huu, saa mbili usiku, polisi walivamia nyumbani kwa Bw. Yusuph Ali na mkewe Bi.Sumaia Juma ambao walikutwa na mabomu yaliyotengenezwa Ujerumani na Urusi.

"Polisi walifanya upekuzi wa kina na kuyakuta mabomu haya yakiwa tayari kwenda kulipuliwa pamoja na vifaa vingine ambavyo vinasadikika kutumika katika ulipuaji mabomu haya," alisema Mngulu.

Aliongeza kuwa, watuhumiwa hao watafikishwa mahakamani muda wowote ili kujibu mashtaka yanayowakabili akiwataja baadhi yao kuwa ni Imamu wa Msikiti huo, Jafari Lema, Shabani Musa, Athumani Hussein, Mohamed Nuru na Abdul Mohamed.

"Bado tunaendelea kumtafuta kinara wa mabomu haya ambaye pia anasadikiwa kuwa ndiye kiongozi wa ulipuaji bomu anayefahamika kwa jina la Yahaya Hassani, kwa sasa ametokomea kusikojulikana.

"Jeshi la Polisi litatoa zawadi nono kwa yeyote ambaye atasaidia kukamatwa kwa Yahaya ili amani ya Mkoa wa Arusha iweze kurudikama ilivyokuwa siku za nyuma," alisema.

Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Arusha Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa